May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Jenerali Mabeyo aweka jiwe la msingi Skimu ya Umwagiliaji JKT

Na Joyce Kasiki,timesmajira online,Chita

MKUU wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Venance Mabeyo ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa Skimu ya Kilimo cha Umwagiliaji katika Kikosi cha 837 Chita JKT kilichopo Wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro.

Jenerali Mabeyo amesema kuanzishwa kwa skimu hiyo ya umwagiliaji ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano za kuzalisha kwa tija ili kuhakikisha Taifa linakuwa na uhakika wa chakula salama kuelekea uchumi wa viwanda.

Ameyasema hayo wakati wa uwekaji jiwe la msingi ujenzi wa miundombinu ya Skimu ya Umwagiliaji inayojengwa katika kambi hiyo.

“Tulizoea tukiwa na njaa tunaagiza chakula kutoka nje, tulizoea kuwatumia wafanyabiashara kutuletea chakula, lakini vile vile tulizoea wakati wa njaa kupata chakula cha msaada. Nadhani tunahitaji sasa kufika mwisho, tunataka tuwe sehemu ya kutoa chakula kwa wanaohitaji chakula ndani na nje ya nchi na kwa eneo hili la Chita hilo linawezekana,”amesema na kuongeza’.

“Kwa sababu nikiwa hapa nimepokea taarifa na historia ya namna ya kilimo mkakati kilivyoanzishwa hadi hapa tulipofikia leo, pia nimejionea mwenyewe kazi ya ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji kwa zao la mpunga ni imani yangu kuwa mradi huu utakamilika kama ulivyopangwa.

“Kama sijasahau mwaka jana wenzetu waliokumbwa na njaa nchi ya Zimbabwe,Kenya na Ruanda walikuja kutafuta chakula kwetu, Akiba ya Taifa ilikuwepo, lakini inawezekana haikuwa ikitosheleza mahitaji ya wenzetu, lakini wakulima wa kawaida kwa kutumia jembe la mkono walikuwa na chakula cha kutosha na kuwahakikishia hawa wenzetu kwamba watapata chakula ,baada ya hapo na sisi kama jeshi tukasema kazi hii tunaiweza.”

Amesema kambi ya Jeshi ya Chita ina eneo la hekari 35,000, lakini hekari hizo hazijatumika kikamilifu, kilimo kinachotarajiwa sasa cha umwagiliaji kinahitaji kuwa na mpango madhubuti kuhakikisha eneo husika linalimwa kwa kubadilisha mazao ya aina mbalimbali.

Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali, Venance Mabeyo akichanganya zege kwenye uzinduzi wa uwekaji jiwe la msingi wa jenzi wa skimu ya kilimo cha umwagiliaji.

“Lazima tuweke mpango madhubuti wa kulima kwa mzunguko kama tunatoa mpunga,msimu mwingine tunatoa mahindi ,msimu mwingine matunda na msimu mwingine mboga.” Amesisitiza

Amesema gharama zote za ujenzi na kilimo zitarejeshwa pale watakapoendelea kujituma katika uzalishaji wenye tija.

“Na mimi niseme kwenye mfuko wa mkuu wa Majeshi natoa milioni 200 ili zisaidie kukamilisha miundombinu na kilimo hiki kitakapoanza kisisimame hata mara moja,”amesema.

Kwa upande wa vijana wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Jenerali Mabeyo amesema ni fursa kwao kuweza kujiajiri kupitia JKT na aliwasisitiza kufanya kazi kwa weledi bila kukata tamaa kwani manufaa makubwa yatapatikana na hatimaye kuweza kuendesha maisha yo popote watakapokuwa

Hadi sasa sekta ya kilimo mifugo na uvuvi vinachangia kwa asilimia 65 ya malighafi ya viwandani nchini na hiyo ni dhahiri kwamba uwezeshaji huo mkubwa wa kilimo cha umwagiliaji utaongeza kiasi cha malighafi inayotumika katika viwanda vyetu, hivyo kupunguza kiasi cha fedha kigeni zinatumika kununulia malighafi nje ya nchi

Amesema kwa muktadha huo amewaomba waoone uwezekano wa kuwekeza katika mazao mengine husA mazao yanayotoa mafuta kama alizeti

Amesema mwaka 2019 /2020 nchi yetu ilitumia sh.bilioni 413 kuagiza mafuta ya kula nje ya nchi wakati mahitaji yetu ya mafuta ni tani 400,000 hadi 520,000 kwa mwaka.

“Uwezo wa ndani ni kuzalisha tani 180,000 kwa mantiki hiyo tuna upungufu wa tani 220 ,000 hadi 340,000 za mafuta ya kula ,changamoto hii ni fursa kwa upande mwingine, ni wajibu wetu sasa kuigeuza hii changamoto kuwa fursa kwa kuwekeza katika kilimo cha mazao yanayozalisha mafuta ya kula ili kiasi cha fedha kinachotumika kuagiza mafuta nje ya nchi kibaki JKT,”amesema na kuongeza;

Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali, Venance Mabeyo, Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT),Meja Jenerali Charles Mbuge na maofisa wa JKT na wataalam kutoka Tume ya Umwagiliaji wakiangalia sehemu ya ujenzi wa mradi wa Skimu ya Kilimo cha Umwagiliaji.

“Uwekaji jiwe la msingi katika ujenzi wa Skimu ya Umwagiliaji wa Kilimo cha mpunga naamini ni kiashiria cha uzalishaji wenye tija kwa historia ya kilimo cha umwagiliaji ndani ya JKT.

Kama mtalima kisayansi,mtavuna zaidi ,tofauti na huko nyuma mimi mwenyewe nilipita JKT mwaka 1978 ulikuwa unapimwa mraba wenye kilomita nzima au zaidi zaidi,hebu angali utalima kitaalam pale ili uumalize huo mraba.”

Kwa upande Mkuu wa JKT Meja Jenerali Charles Mbuge, amesema mradi huo unatekelezwa na wataalam wa haap nchini ambao wamejengewa uwezo kufanya kazi hi

“Tunashukuru kwa kuwajengea uwezo maofisa askari kwenda kusoma ili waweze kufanya kazi hii ambayo siku za nyuma wataalam walitoka nchi za nje kwa kushirikiana na wataalam wa ndani.”amesema Meja Jenerali Mbuge