March 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wachezaji yampasua kichwa Kaze, kupitisha panga kwa washambuliaji

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

UBUTU wa safu ya ushambuliaji ya klabu ya Yanga umeendelea kumpasua kichwa kocha mkuu wa timu hiyo Cedric Kaze ambaye amethibitisha kuwa huenda akawafyeka baadhi ya nyota wake ili kuongeza wengine wapya katika Dirisha Dogo la usajili litakalofunguliwa Desemba 15.

Kaze ametoa kauli hiyo baada ya kutoridhishwa na matokeo ya goli 1-0 katika mchezo wao uliochezwa juzi kwenye uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam dhidi ya Maafande wa JKT Tanzania.

Toka kocha huyo ameanza kuliongoza benchi la ufundi la Yanga katika mchezo dhidi ya Polisi Tanzania uliochezwa Oktoba 22, timu hiyo ilifanikiwa kufunga goli 2-1 katika mchezo mmoja tu dhidi ya KMC huku wakitoka sare na kuendeleza ushindi wa goli moja.

Licha ya wiki iliyopita kocha huyo kuweka wazi kutozungumzia mambo yoyote ya usajili hadi pale utakapofunguliwa rasmi lakini kilichomuumiza ni wachezaji wake kupoteza nafasi za wazi ambazo zingeweza kuwapa ushindi hata wa zaidi ya goli tatu.

Kocha huyo amesema, katika kipindi cha kwanza cha mchezo wao dhidi ya JKT, walipata nafasi za wazi tatu na wachezaji wake walishindwa kuzimalizia lakini walikuwa wakiwaachia wapinzani wao hadi katika eneo la hatari na kufanya mashambulizi kwa urahisi.

Kipindi cha pili mchezo huo ulikuwa mgumu zaidi lakini waliweza kuzuia mashambulizi na kufanikiwa kupata alama tatu hivyo japokuwa wapo kileleni mwa msimamo wa ligi lakini bado wana vitu vingi vya kurekebisha.

Amesema, kwa sasa wanatakiwa kutuliza akili na kufanya tathmini kuangalia kama wachezaji hao wanatakiwa kupewa mbinu nyingine zitakazowafanya kutumia nafasi za kupachika magoli au kutafuta wachezaji wengine ambao wataweza kuleta mabadiliko ndani ya kikosi.

“Leo nakubali kuwa safu yangu ya ushambuliaji ina shida kubwa kwani naamini kuwa katika mechi mbili au tatu za nyuma tungeweza kuzimaliza mapema mchezo tena kwa zaidi ya goli moja lakini kadri dakika zinavyokwenda ndivyo wachezaji wangu wanakaribisha presha ya mchezo kwa kufanya makosa mengii madogo madogo na kuwafanya wapinzani wetu kuongeza kujiamini na kutuweka shakan, ” amesema kocha Kaze.

Akizungumzia kiwango ya mchezaji bora wa mechi hiyo kwa mujibu wa mashabiki wa Yanga, Deus Kaseke aliyepata kwa wastani wa asilimia 65 ya kura na kuwabwaga Yassin Mustapha na Tuisila Kisinda ambaye amekuwa bora ka kuipa ushindi katika mechi mbili zilizopita, kocha huyo alisema kuwa, Kaseke ni mchezaji anayejua wapi anatakiwa kuwepo kwa muda sahihi.

Pia ni mchezaji mwenye uwezo wa kutoka nyuma na kwenda hadi ndani ya boksi bila watu kutegemea mabaye walikuwa wakimkosa siku za nyuma ndani ya kikosi chake.

“Washambuaji wanapokuwa ndani ya boksi mabeki wote wanawaangalia lakini ameonesha uwezo kwani ameweza kukimbia kutoka nyumba na kuingia kwenye boski na kuleta madhara ambaye tulikuwa tukimkosa,” amesema Kaze.