May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCM Ilemela yakemea makundi CCM, yampongeza Dkt. Angeline kuchaguliwa NEC – CCM

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Ilemela Yusuph Bujiku,amekemea makundi ndani ya chama pamoja na kuhakikisha Serikali inasimamiwa vizuri.

Huku chama hicho wilayani Ilemela kikitoa pongezi kwa Mbunge wa Jimbo la Ilemela Dkt.Angeline Mabula kwa utekelezaji wa shughuli za maendeleo jimboni humo pamoja na kushinda nafasi ya ujumbe wa Halmashauri Kuu taifa kupitia Uchaguzi Mkuu wa CCM uliofanyika hivi karibuni.

Bujiku amezungumza hayo wakati wa muendelezo wa ziara yake ya kukagua uhai wa chama na kuhamasisha ujenzi wa ofisi za chama hicho kwa ngazi ya matawi na kata akiwa katika Kata za Kahama na Nyamh’ongolo.

Ambapo amekemea makundi ndani ya chama na kuwataka viongozi waliochaguliwa hivi karibuni kwa ngazi ya matawi na kata kuhakikisha wanatekeleza wajibu wao ipasavyo. Kwani hatavumilia kiongozi yeyote asiyetimiza wajibu wake ikiwemo kufanya ziara za kukagua utekelezaji wa Ilani na uimarishaji wa chama.

“Uchaguzi wa Chama kwa ngazi ya taifa kwa mwaka huu Ilemela tuna la kujivunia…,tumepata Mjumbe wa Halmashauri Kuu Taifa (Mnec) kutoka ndani ya wilaya yetu, tumpongeze na tujivunie,”ameeleza Bujiku.

Mwenyekiti wa CCM Kata ya Kahama Mathayo Nocholaus, ameeleza kuwa katika kipindi chake Cha uongozi hataacha kuisimamia Serikali ili kuhakikisha kilichoahidiwa na chama kwa wananchi kwa kipindi cha miaka mitano kinatekelezwa huku watendaji wavivu hawana nafasi ndani ya kata hiyoKwa upande wake Katibu wa CCM Kata ya Kahama Luhela George,amefafanua kuwa katika jitihada za ujenzi wa ofisi za matawi na kata wanachama wa CCM Kata ya Kahama mpaka sasa wameshachangia zaidi ya laki 3(343,000)huku zoezi hilo likiendelea kuhakikisha ofisi zinajengwa kila tawi na kata.

Mmoja wa wanachama wa CCM Kata ya Kahama Farida Joachim ameipongeza kamati ya siasa ya wilaya hiyo kwa kuamua kufanya ziara ngazi za matawi na kata ili kukiimarisha chama hicho na kutoa morali kwa viongozi wengine waweze kutimiza wajibu wao huku akisema ziara hizo ziwe endelevu.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Ilemela Yusuph Bujiku akizungumza na wanachama wa CCM Kata ya Kahama, wilayani Ilemela.
Wanachama wa CCM Kata ta ya Kahama wakimsikiliza Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Ilemela Yusuph Bujiku.