May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Zaidi ya watu 2000 kushiriki tamasha la Jinsia Dar

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

WATU zaidi ya 2000 wakiwemo wawakilishi wa Asasi za kiraia kutoka ndani na nje ya nchi wanatarajiwa kushiriki katika Tamasha la 15 la Jinsia ambalo linatarajia kufanyika Novemba 7 hadi 10 mwaka huu katika Viwanja vya Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) Jijini Dar es salaam.

Katika Tamasha hilo mgeni rasmi anatarajia kuwa Aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la UN Women duniani na Makamu wa Rais wa Afrika Kusini Dkt.Phumuzile Mlambo Ngeuka .

Hayo yamebainishwa Jijini Dar es salaam Novemba 5,2023 na Mwenyekiti wa Bodi wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) Gemma Akilimali wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Amesema wageni kutoka nchi 14 kutoka mabara matatu duniani wanatarajiwa kushiriki katika tamasha hilo.

Akitaja nchi hizo ni pamoja na Ghana, Canada, Korea Kusini, India, Haiti, Eswatini, Afrika Kusini, Ethiopia, Zambia, Zimbabwe, Bangladesh, Uganda, Kenya na Tanzania.

” Tamasha hili linatambulisha mifumo iliyopo ya uchumi inayounga mkono mapambano ya wanawake na wanaharakati wa ukombozi wa wanawake wanaotaka ugawaji wa haki na usawa wa rasilimali ikiwamo ya maji bajeti za kuhudumia huduma za kijamii, rasilimali asilia kama ardhi, misitu na nafasi za uongozi na upatikanaji wa haki kwa watu wote”

Gemma amesema tamasha hilo litahusisha mawasilisho, mijadala ya moja kwa moja, maonesho na warsha mbalimbali. Mijadala ya pamoja itajenga dhana halisi kuhusu mada ndogo katika siku husika.

Vilevile amesema Maonesho yatafanyika siku zote za Tamasha , yakitoa fursa kwa TGNP, taasisi na mitandao mingine inayoshiriki kubadilishana ujuzi kupitia vyombo vya habari (video, mabango na picha).

“Wachapishaji, azaki na wasanii wa kike wanahimizwa kuonyesha na kuuza bidhaa zao ambapo jumla ya taasisi na mitandao mingine 42 zimeshajiandikisha kuonyesha kazi zao siku zote za Tamasha”amesema Gemma.

Pamoja na hayo amesema kutakuwa na tuzo ya heshima ambapo mama zetu, kinadada, mabinti watakumbukwa kwa mchango wao katika mapambano ya kutetea haki za wanawake, usawa wa kijinsia na haki za kijamii.

Naye Mkurugenzi wa TGNP, Lilian Liundi amesema ndani ya miaka 30 ya TGNP kuna mafanikio makubwa yameibuliwa ikiwemo kuleta chachu ya uchambuzi wa kina wa kijinsia .

“TGNP imeongeza uelewa mpana kwa wanawake, taasisi mbalimbali pamoja na wanaume”amesema

Amesema Kupitia mafunzo ya uchambuzi wa kijinsia yamesaidia kwa kiasia kikubwa kuleta sauti na nguvu ya pamoja kupitia majukwaa na mitandao.

“TGNP ilikuwa ni asasi ya kwanza kuanzisha mitandao ya sauti ya pamoja”, amesema Liundi

Mwenyekiti wa bodi Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) Gemma Akilimali akizungumza na waandishi wa habari awapo pichani.
Mkurugenzi wa TGNP, Lilian Liundi akizungumza na waandishi wa habari juu ya Tamasha la 15 la Jinsia ambalo linatarajia kuanza kesho katika Viwanja vya TGNP mtandao mabibo Jijini Dar es salaam