July 19, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watuhumiwa kumshambulia mzee kisa imani za kishirikina

Na Judith Ferdinand, Timesmajira Online-Mwanza

WATU wawili wamekamatwa na wanaendelea kuhojiwa na Jeshi la Polisi mkoani Mwanza kwa tuhuma za kumjeruhi Mihayo Budaga(78), mkazi wa Kitongoji cha Nyambono, kijiji cha Kisamba, Kata ya Lubugu wilayani Magu mkoani humo.

Akizungumza Julai 18,2026 mkoani humo,Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza DCP.Wilbord Mutafungwa,amesema tukio hilo  lilitokea Julai 11,2026 majira ya saa 08:00 usiku,ambapo  Budaga akiwa amelala nyumbani kwake, ghafla watuhumiwa hao ambao ni Lusana Kaswahili na Mbizo  Kaswahili walivamia makazi yake.

Na baada ya hapo watuhumiwa  hao  walivunja mlango wa kuingilia na kuelekea moja kwa moja hadi kwenye chumba chake.

Watuhumiwa hao wakiwa ndani, walimshambulia mzee huyo na kumjeruhi kwa kumkata na kitu chenye ncha kali kichwani  upande wa kulia, pamoja na maeneo mbalimbali ya mkono wake wa kulia na kusababisha  kuvuja damu nyingi na hali yake kiafya kuwa mbaya.

DCP.Mutafungwa amesema,baada ya jeshi hilo  kupokea taarifa hizo, askari walifika haraka eneo la tukio walimchukua majeruhi na kumkimbiza katika Hospitali ya Wilaya ya Magu kwa matibabu lakini kutokana na hali yake kuwa mbaya, alihamishiwa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Bugando ambapo kwa sasa anaendelea vizuri.

Hata hivyo amesema,uchunguzi wa awali umebaini kuwa chanzo cha tukio hilo ni imani za kishirikina na kulipiza kisasi kwani watuhumiwa walikuwa wanamtuhumu Mihayo Budaga, kuwa anawaloga  ndugu zao.

Aidha amesema,watuhumiwa wanaendelea kuhojiwa kwa kina na upelelezi ukikamilika, watafikishwa mahakamani haraka iwezekanavyo ili sheria ichukue mkondo wake

“Natoa rai kwa wananchi wote wanaoendeleza tabia ya  kujichukulia sheria mkononi na kushambulia watu kwa visingizio vya imani za kishirikina au visasi waache mara moja kwani vitendo hivyo havitafumbiwa macho hata kidogo,”amesema DCP.Mutafungwa.

      Â