March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wabunifu kutoana jasho Swahili Fashion Week

Na Angela Mazula, TimesMajira Online

WABUNIFU na wanamitindo mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi watatoana jasho katika jukwaa kubwa la maonyesho ya mavazi na mitindo Afrika Mashariki na Kati la ‘Swahili Fashion Week’ ambalo litafanyika kwa mara ya 13.

Akizungumza kuelekea kwenye onesho hilo litakaloanza Desemba 4, muandaaji wa shindano hilo, Mustafa Hassanali amesema jukwaa hilo litajumuisha weabunifu wa ndani na nje na tayari washiriki wanaotoka nje ya Dar wameshaanza kuwasili kwa ajili ya kushiriki na kushuhudia jukwaa la maonyesho haya maarufu ambayo yatafanyika kwa muda wa siku tatu.

Hassanali ambaye pia ni Muasisi wa Swahili Fashion Week amesema, Mwaka huu kuna wabunifu 56 kutoka ndani na nje ya Tanzania ambao wataonyesha ubunifu wao kwenye jukwaa hilo, wapo wabunifu mbalimbali kutoka Mikoa tofauti Tanzania, kama vile Moshi, Kahama, Arusha, Tanga na Zanzibar.

“Tuna wabunifu kutoka Ulaya, Ghana, Burundi, Kenya na Italia na wengine kutoka nje tayari wameshafika Dar na wanajiandaa kwa shauku kubwa kuonesha ubunifu wao na kazi zao kwenye jukwaa hili la Swahili Fashion Week,”.

“Imebaki siku moja kuanza rasmi na mpaka sasa maandalizi yamekamilika hivyo nawakaribisha wote ambao wamesafiri kutoka nchi mbalimbali kwa ajili ya kushiriki, kushuhudia na kuwa sehemu ya maonyesho haya kwani ubunifu wa mavazi ni kazi kama kazi zin gine tuu,” amesema Hassanali.

Hata hivyo amesema kuwa, katika siku hizo tatu za maonesho watu furahia mitindo, urembo, pamoja na miondoko ya wanamitindo waliojiandaa vizuri jambo litakaloendelea kuiweka Tanzania juu zaidi kwenye tasnia ya ubunifu na uwanamitindo ‘Tanzania Unforgetable’.