April 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Pawasa awasoma wapinzani michuano ya mataifa Afrika

Na Yusuph Digossi, TimesMajira Online, Dar es Salaam

KOCHA Mkuu wa Timu ya Taifa ya Tanzania ya Soka ya Ufukweni ‘Beach Soccer’, Boniface Pawasa amesema tayari wameshaanza kupitia video kadhaa za wapinzani wao waliopangwa nao kundi moja katika Fainali za Kombe la Mataifa Afrika (BSAFCON 2021) zitakazoanza kutimua vumbi Mei 23 hadi 29 nchini Senegal.

Katika michuano hiyo Tanzania imepangwa Kundi A pamoja na wenyeji Senegal, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo.

Tanzania itatupa karata yake ya kwanza dhidi ya majirani zao Uganda kisha watakuwa wageni wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo na kumaliza na wenyeji Senegal ambao watafungua dimba katika michuano hiyo na Congo.

Akizungumzia maendelea ya kikosi chake Pawasa amesema kuwa, baada ya mazoezi ya kujenga utimamu na wakiwa wamemaliza sehemu kubwa ya mazoezi awamu ya pili ya programu ambayo imejikita zaidi kwenye mbinu za kiufundi, ujanja na ubunifu, wameshaanza maalizi ya wiki ya mwisho ambayo itajikita zaidi katika mechi za kirafiki.

Mechi hizo zitawasaidi kuonesha mapungufu yaliyopo katika kikosi chao lakini pia kuwawezesha kufanya tathmini ni hatua gani wamefika kuelekea katika fainali hizo ambazo wamepania kufanya kazi nzuri.

Kocha huyo amesema kuwa, hadi sasa wameshapitia video kadhaa za wapinzani wao ili kuweza kusoma mbinu zao, wanachezaje na wanatumia mtindo gani katika kushambulia na kujilinda ili kuweza kuwapa urahisi.

“Tayari tumeshaanza maandalizi ya wiki ya mwisho ya mazoezi yet una tunaendelea na kazi ya kuzichambua video za wapinzani wetu ili kuona mbinu zao , kuona wanachezaje, mbinu wanazotumia katika kushambulia na kujilinda pamoja na kukagua ubora na mapungufu yao,” amesema Pawasa.

Itakumbukwa kuwa hii ni mara ya pili mfululizo Tanzania inafuzu kucheza fainali hizo baada ya mwaka 2018 kufanikiwa kufanya vizuri baada ya kudika nafasi ya nane katika ya nchi 52 katika viwango vya Afrika na dunia.

Tanzania ilifanikiwa kufuzu fainali hizo baada ya kupata ushindi wa jumla wa goli 12-9 wakifanikiwa kushinda goli 8-3 katika mchezo wa kwanza na kufungwa goli 6-4 katika mchezo wa marudiano uliochezwa Aprili 3 kwenye fukwe za Coco.