April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Nyaraka za usimamizi wa maafa zazinduliwa kudhibiti kabla ya majanga kutokea

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali imeanzisha kituo  cha oparesheni na mawasiliano ya dharura katika ngazi  ya Taifa na vituo vya kisekta ili kuratibu oparesheni zote za maafa .

Akizungumza leo Februari 9,2023 muda mfupi kabla ya kuzindia nyaraka za usimamizi wa maafa Majaliwa amesema kituo hicho kitawezesha upatikanaji wa taarifa zinazohusiana na maafa ili kuchukua hatua mapema kabla maafa hayajatokea.

Amesema,mifumo ya tahadhari ya hali ya hewa ni vyema ianishwe na kuwezesha upatikanaji wa vituo vya kutosha  na vya kisasa vya hali ya hewa na kuwezesha mipango na kujiandaa kukabiliana na maafa na ngazi ya wilaya pamoja na kutoa elimu  kwa umma kuhusu masuala ya usimamizi wa maafa nchini.

Vile vile amesema Serikali imeanza ujenzi wa kituo cha maafa cha kudumu katika eneo la nzuguni jijini Dodoma.

“Kukamilika kwa  kituo hicho kutawezesha ufanisi zaidi katika kuratibu oparesheni za maafa na kuimarisha huduma za binadamu kwa waathirika wa maafa,kwa sasa angalau kila ofisi ya mkoa ina mitambo inayoweza kutabili hali ya hewa kwenye mkoa husika na kuwezesha kamati ya maafa mkoa kujiandaa kutokana na taarifa hizo .”amesema na kuongeza kuwa

“Sasa hatupaswi kuishia mkoani tu vifaa hivi vipatikane mpaka kwenye halmashauri wakati mwingine wilaya moja hadi nyingine zina hali ya hewa tofauti .”

Ametumia nafasi hiyo kuzitaka Sekta zote zinazohusika na utekelezaji wa shughuli za usimamizi wa maafa kuhakikisha kuwa zinawajibika kikamilifu katika kushughulikia dharura inapotokea wakati wowote.

Amezitaka sekta na taasisi husika kufanya  tathimini  na kugundua ni vitu gani vinasababisha majanga katika jamii na kuyadhibiti mapema .

Aidha amezitaka Taasisi zinazoshughulikia masuala ya maafa ziweke mipango ya dharura katika maeneo yao ili kudhibiti magonjwa ya mlipuko au ya maambukizi ambayo hasa yanatoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu .