April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mwinuka aibuka kidedea ‘NMB Lugalo Proffessionals Tour 2021’

Na Penina Malundo, TimesMajira Onlinemichuano ya

NYOTA wa kulipwa wa mchezo wa Gofu kutoka klabu ya gofu Lugalo, Frank Mwinuka ameibuka kidedea katika michuano ya mchezo wa gofu iliyoshirikisha wachezaji wa kulipwa ‘NMB Lugalo Proffessionals Tour 2021’.

Katika mashindano yaliyoshirikisha wachezaji kutoka klabu mbalimbali, Mwinuka alipiga Mikwaju 146, nafasi ya pili ikichukuliwa na Elsant Lembris aliyepiga mikwaju 148 huku Nuru Mollel akiishikilia namba tatu kwa mikwaju 148 wakitokea Klabu ya Gykhana ya Arusha.

Mashindano hayo yalisindikizwa na zaidi ya wachezaji 100 wa ridhaa ambapo katika kundi la ‘Junior’, Salehe Ramadhani wa Lugalo aliibuka mshindi wa kwanza kwa kupiga Mikwaju 75 huku nafasi ya pili ikichukuliwa na Shufaa Twalib Aliyepiga Mikwaju 79.

Akizungumza baada ya kumalizika kwa mashindano hayo, Mwenyekiti wa klabu ya Lugalo, Brigedia Jenerali Mstaafu, Michael Luwongo amesema kuwa, mashindano hayo yalikuwa yanalenga kuinua vipaji vya wachezaji hao kwani bado klabu hazijaweza kuiwakilisha Tanzania vizuri katika mashindano ya kimataifa.

Jambo hilo limekuwa likiwafanya kushindwa kupelekewa wawakilishi kwani hata wao kama viongozi bado hawajajiamoni kuwa wanaweza kupeleka wawakilishi katika mashindano yanayoandaliwa na nchi jirani kwa kuogoipa kurudi na ambacho hawajakitarajia.

“Ili tujiamini inabidi kuwaandae wachezaji wetu na ndio maana tumeandaa mashindano haya kwani hatutaki waishie tu kuwa wakufunzi wa hapa klabu bali wafikie viwango vya kuwa washindani katika ngazi za kimataifa ili hapa tutakapopata mwaliko tusisite na tupeleke washindani zaidi ya watatu,”.

“Huu ni mwanzo lakini pia tujitathmini kwa kuanzia hapa hapa ndani ya klabu na kujiuliza je, matokeo tunayoyapata yanafanana na yale wanayoyayapata washindani wetu kutoka nje? Na takwimu tunazozikusanya zitusaidia kuona kama tumefanya maandalizi mazuri na sasa tumepanga kuwa na mashindano mengi ya aina hii ili kuweza kuzalisha wachezaji bora ambao watatuwakilisha vema kimataifa,” amesema Jenerali Mstaafu, Michael Luwongo.

Aidha amewataka wachezaji hao wa kulipwa kujitahidi kupandisha viwango na kutoridhika na matokeo wanayoyapata hapa nyumbani kwani klabu ina uwezo wa kupeleka wachezaji zaidi ya watatu nje ya nchi na ndio maana wanataka kukazania katika mashindano ili kukuza viwango.

Hata hivyo amewapongeza watoto walioshiriki mashindano hayo kwa uthubutu wa hali ya juu waliouonyesha kwani licha ya watoto hao kushiriki katika mazingira magumu mashindano hayo lakini wamejitahidi kwa kiasi kikubwa kufanya vizuri.

“Nawashukuru Junior wote katika shindano hili najua mmeshiriki katika mazingira magumu lakini mmejitahidi, nawachukulia nyie ndio wenye hii klabu hakikisheni mnaendelee kukua hadi hapo mtakapokuwa wakubwa ambapo mtaifahamu vizuri sana kwani rika lenu ni msingi mzuri katika kujua mchezo huu hivyo hamtakiwi kuacha mazoezi  na mjitahidi ili mje kuwa wachezaji wazuri zaidi,”amesema jenerali Mstaafu Michael Luwongo