March 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

MSD yatumia bil 16.7 kiwanda gloves na dawa Idofi Makambako

Erick Mapunda Mkurugenzi wa Utawala na Rasirimali Watu Bohari ya Dawa (MSD) akisikiliza Meneja wa Mawasiliano Bohari ya Dawa MSD Bi. Etty Kusiluka akuzungumza na waandishi na kutoa utaratibu wa namana ziara itakavyofanyika kiwandani hapo kabla ya waandishi kuanza kutembelea mradi huo, , Kulia ni Catherine Sungura Mratibu wa Shughuli za Maendeleo Mwaka mmoja wa Rais Samia Suluhu Hassan madarakani kutoka Wizara ya Afya na kushoto ni Shiwa Mushi Mhandisi Msimamizi Miradi ya Viwanda MSD.

Erick Mapunda Mkurugenzi wa Utawala na Rasirimali Watu Bohari ya Dawa (MSD) akizungumza na waandishi wa habari kabla ya kuanza ziara ya kutembelea kiwanda cha Bohari ya Dawa MSD kinachojengwa eneo la Idofi Makambako mkoani Njombe kutoka kulia ni Catherine Sungura Mratibu wa Shughuli za Maendeleo Mwaka mmoja wa Rais Samia Suluhu Hassan madarakani kutoka Wizara ya Afya, Meneja wa Mawasiliano Bohari ya Dawa MSD Bi. Etty Kusiluka na kushoto ni Shiwa Mushi Mhandisi Msimamizi Miradi ya Viwanda MSD.

………………………

Bohari ya Dawa MSD inaendelea na ujenzi wa kiwanda Cha mipira ya mikono (Glaves) na Dawa katika eneo la Idofi Makambako mkoani Njombe ambapo mpaka sasa imetumia zaidi ya shilingi za kitanzania Bilioni 16.7 kununua mitambo, ujenzi wa majengo na miundombinu.

Kiasi Cha shilingi Bilioni 15.56 zimetolewa na serikali na kiasi kilichobaki kimechangiwa na hazina ikiwemo mapato ya ndani ya MSD pamoja na wadau wengine ambapo ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 90% huku kazi ya ufungaji wa mitambo ikiendelea.

Hayo yameelezwa na Erick Mapunda Mkurugenzi wa Utawala na Rasirimali Watu Bohari ya Dawa (MSD) ambapo amesema mradi wa ujenzi huo viwanda vya dawa na vifaa tiba, ulianza rasmi Aprili 4 Oktoba, 2020 kwa lengo la kuanzisha kiwanda cha Mipira ya mikono (gloves).

Amefafanua kuwa wazo hilo lilitokana na changamoto ya upatikanaji wa bidhaa hiyo wakati huo, kutokana na anga nyingi duniani ambazo MSD inategemea kuagiza bidhaa hiyo zilikuwa zimefungwa hivyo MSD ikaamua kuchukua maamuzi ya kujenga kiwanda hiki.

Aidha amesema kutokana na janga la Uviko 19, baadhi ya wataalamu wa kufunga mitambo kutoka China walichelewa kuwasili nchini hivyo kuathiri ukamilishaji wa ufungaji wa mitambo.

Ameeleza kuwa Kwa sasa ujenzi wa majengo ya viwanda vya dawa za vidonge, dawa za maji na vidonge vya rangi mbili, unaohusisha ujenzi wa majengo matatu yanayofanana kwa ukubwa yenye mita za mraba 900 (urefu mita 50.8, upana mita 17.7 na kimo cha mita 7) kwa kila jengo ufungaji wa mitambo unaendelea.

“Mpaka sasa ujenzi wa majengo yote matatu umekamilika kwa asilimia 90% na unatarajiwa kukamilika katika robo ya tatu ya mwaka 2022,” Amesema Bw. Erick Mapunda.

Aidha amefafanua kwamba Upokeaji wa mitambo ya kuzalisha Syrup (Vimiminika) Rangi mbili (Capsule) na dawa umekamilika kwa asilimia mia 100% mpaka mwezi Desemba, 2021 ambapo ufungaji wa mifumo ya maji na mitambo pamoja na eneo la usafi (Clean Room) unaendelea.

Akielezea zaidi kuhusu mradi huo amesema MSD pia imenunua mitambo ya kutengeneza na kufungasha dawa rojorojo (Ointment and Cream); ambayo imekwishawasili nchini katika eneo la mradi MSD Keko makao makuu ambapo manunuzi ya mitambo na malighafi ya ujenzi wa kiwanda yamekamilika kwa asilimia 60% huku Ukarabati wa jengo la kiwanda ukiwa umefikia asilimia 60% ambao unatarajiwa kukamilika mwaka huu 2022.

Akizungumzaia upatikanaji wa malighafi ya utomvu aina ya Latex kwa ajili ya kutengenezea Mipira ya mokono (Glaves) katika kiwanda hicho amesema juhudi za kutafuta malighafi hiyo maeneo ya Tanzania Bara zinaendelea.

“Hata hivyo, jitihada zinaendelea ili kupatiwa mashamba ya miti (aina ya Rubber) kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. mazungumzo yanaendelea kwakuwa upatikanaji wa malighafi hii ndani ya nchi utapunguza gharama za kuagiza za kutoka nje ya nchi,” Amesema Erick Mapunda.

Akizungumzia uzalishaji amesema Dawa na vifaa tiba vinavyotarajiwa kuzalishwa kwenye viwanda vinavyojengwa eneo la Idofi ni kwamba Kiwanda cha Vifaa Tiba kitazalisha Sugical na Examination Gloves ambapo gloves 20,000 zitazalishwa kwa saa,sawa na jozi 10,000 kwa saa.

Amefafanua kuwa viwanda vya Vidonge na Rangimbili (Tablets) vyenyewe vitazalisha 330,000 kwa saa na vidonge vya kawaida (Capsules) vitazalishwa 425,000 kwa saa ambapo dawa hizo ni aina ya Paracetamol, Amoxycillin, Arythromycin, Ampiclox.

“Kiwanda cha dawa za maji (Syrup) kitazalisha jumla ya chupa 180 kwa saa na dawa hizi ni pamoja na Cough Syrup, Paracetamol Syrup, Cotrimoxazole Syrup na Metronidazole syrup,” Amesema Erick Mapunda.

Ameongeza kuwa Menejimenti ya MSD inatambua mchango kutoka serikalini kwa kuwezesha ujenzi wa viwanda vya uzalishaji wa dawa na vifaa tiba unaofanywa na MSD hivyo ametoa shukurani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe, Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha za utekelezaji wa ujenzi wa viwanda hivyo vya uzalishaji wa dawa

Ameshukuru pia Wizara ya Afya kwa kufanikisha mipango yote ya miradi hii na kufuatilia kwa karibu maendeleo yake. zikiwemo taasisi mbalimbali kama vile TMDA, Mkemia Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha na Mipango, TANESCO, TANROADS, NEMC, TARURA, DAKWASO, Wizara ya Mambo ya Ndani, JWTZ na SUMA JKT.

Bw. Erick ametoa shukurani za kipekee kwa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Njombe, ikiongozwa na Eng. Marwa Rubirya kwa kuwezesha kupata ardhi na kusimama na MSD katika mchakato mzima wa kuwezesha mradi wakiwemo wananchi wa Kata ya Mlowa, Idofi Makambako ambako ndiko mradi huu unatekelezwa.

Shiwa Mushi Mhandisi Msimamizi Miradi ya Viwanda MSD akitoa maelezo kwa waandishi wa habari waliotembelea kiwanda cha dawa cha Idofi Makambako mkoani Njombe wakati walipotembelea kwanda hicho na kujionea shughuli za ujenzi zinavyoendelea kiwandani hapo.

Shiwa Mushi Mhandisi Msimamizi Miradi ya Viwanda MSD akionesha kwa waandishi wa habari mitambo ambayo imeshafungwa kiwandani hapo tayari kwa ajili ya kuanza shughuli za uzalishaji.

Baadhi ya mitambo inavyoonekana.

Baadhi ya mafundi wakiendelea na kazi ya ufungaji wa mitambo hiyo.

Baadhi ya kitambo ya kusafisha na kuangalia ubora wa vifaa tiba.

Mtambo kwa ajili ya gesi ya kuendeshea baadhi ya mitambo kiwandani hapo.

Moja ya Majengo ya kiwanda hicho linavyoonekana.

Moja ya nyumba za watumishi wa kiwanda hicho.