April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Balozi wa Msumbiji ahimiza vijana wa Kitanzania kuendeleza talanta zao

Mwandishi Wetu,TimesMajira,Online,Dar

BALOZI wa Msumbiji nchini, Ricardo Amrosio Mtumbuida, amewataka vijana nchini kujenga tabia ya kuziendeleza talanta zao kama njia mojawapo ya kujipatia kipato cha uhakika na kuondokana na dhana ya kusubiri kuajiriwa.

“Wakati umefika kwa vijana kuanza kuzitambua talanta ambazo Mungu amewapa na kuzibadilisha kuwa fursa ambazo zitawasaidia kubadilisha maisha yao sambamba na kuondoka na dhana ya kusubiri kuajiriwa,” amesema Balozi Mtumbuida.

Akizungumza jijini Dar es Salaam kwenye hafla ya uzinduzi wa vitabu viwili vya kiingereza vya ‘A day with a Quote na Dear Paula’ ambavyo viandikwa na Mshairi chipukizi, Aisha Kingu alisema ni wakati wa vijana kutumia talanta zao kujiajiri ili wajikwamue kiuchumi kwani zipo fursa nyingzimefichwa kwenye talanta za vijana.

Ametoa wito kwa wazazi kuwa mstari wa mbele kuhakikisha wanazitambua talanta za watoto wao na kuziendeleza ili ziwe mkombozi kwa siku za usoni kwa kujitengenea kipato cha uhakika.

“Wazazi wapo katika nafasi nzuri sana ya kuziendeleza talanta za watoto wao tangu wanapozaliwa. Napenda pia kumpongeza Dkt. Saidi Kingu kwa kutambua talanta ya binti yake na kumsaidia kufikia malengo na kutimiza ndoto zake,” amesema.

Kwa upande wake, Mwandishi wa Vitabu hivyo, Aisha amesema vitabu hivyo vimebeba ujumbe mbalimbali na kila atakayesoma vitabu hivyo vitampa msukumo na nguvu yakukabiliana na changamoto pamoja na mtazamo chanya katika kufikia mafanikio.

“Ukiangalia kitabu cha Dear Paula, ni kitabu kilicholenga kumpatia uhuru wa kipato binti kupitia usajiriamali ambapo tunaona barua ya mama kwenda kwa mtoto inayompa muongozo na njia katika safari ya ujasiriamali sambamba na kumkumbusha yeye ni nani na anapaswa kufanya nini ili kufikia mafanikio,” alisema Aisha na kuongeza kuwa A Day with a Quote ni kitabu ambacho ambacho kimebeba dhima ya msukumo , kutia moyo na motisha .

Balozi wa Msumbiji nchini Tanzania, Ricardo Amrosio Mtumbuida, (katikati) akizindua vitabu vya A day with a Quote na Dear Paula vilivyoandikwa na Mshairi chipukizi, Aisha Kingu (watatu kushoto) kwenye hafla ya uzinduzi iliyofanyika Jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Wapili kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya ushindani wa haki (FCC) William Erio.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani wa Haki (FCC) William Erio amewapongeza wazazi wa binti huyo na kushauri wazazi wengine kuiga mfano huo na kuwa chachu katika kuendeleza vipaji vya watoto wao, kwani kwa kufanya hivyo watoto watapa uhuru na ufanisi zadi kiutendaji badala ya kuwalazimisha kufanya wasiyoyataka.

“Nipende kuwaasa wazazi wezangu kuiga mfano wa wazazi wa Aisha Kingu kwani walitambua talanta ya binti yao na kuiendeleza na sasa amekuwa akipeperusha bendera ya Tanzania ndani na nje ya Tanzania kwa talanta tu,” Amesema Erio.

Aisha mbali ya kuwa mwandishi wa vitabu na mtunzi wa mashairi ni mwanasheria na wakili pamoja umri wake mdogo amejizolea umaarufu mkubwa kwa kuwaandikia mashairi viongozi wa ndani ya nchi na nje ya Tanzania akiwemo Rais mstaafu wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Urusi Vladimir Putin na Malikia Elizabeth wa Uingereza.