April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Maandalizi Karume Cup yanoga

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

CHAMA cha Mpira wa Kikapu visiwani Zanzibar (BAZA) kimesema kimefikia hatua nzuri kwenye maandalizi ya michuano ya mpira wa kikapu ya Kombe la Karume ‘Karume Cup’ iliyopangwa kuendelea Mei 16 katika viwanja vya Mao ze Dong na Maisara.

Itakumbukwa kuwa, BAZA walisitisha michuano hiyo kupisha siku 21 za maombolezo ya kifo cha aliyekuwa rais wa Awamu ya Tano ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli kilichotokea Machi 17.

Lakini baada ya kumaliika kwa siku hizo za maombolezo, viongozi za BAZA waliamua kuendelea kusimamisha mashindano hayo kutokana na kubakiza siku chache kabla ya kuanza kwa mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramandani.

Makamu Mwenyekiti wa BAZA, Rashid Hamza Khamis, ameuambia Mtandao huu kuwa, wakati wanatoa tarehe mpya za mashindano hayo walikuwa wameshaanza maandalizi ambayo sasa yapo katika hatua nzuri na wanaamini yatafanya muendelezo wa michuano hiyo kuwa na msisimko mkubwa.

Amesema, toka awali mkakati wao ulikuwa ni kutoa mapema ratiba hiyo na baada ya vikao kadhaa walikubaliana Ligi huyo kuendelea Mei 16 na kuhitimishwa kwa mchezo wa fainali utakaochezwa Mei 25.

“Katika mechi zitakazochezwa Mei 16, New West atawakabili Nyuki huku Usolo ikivaana na Millennium na Mei 17 timu za wanawake, New West watawakaribisha KVZ huku KZU wakipambana na JKU,”.

“Baada ya hatua hiyo ya makundi mshindi wa kwanza wa Kundi A atacheza dhidi ya mshindi wa pili wa kundi B wakati wa kushindi wa kwanza wa kundi B atavaana na mshindi wa kundi A na kisha washindi watachuaka kusaka washindi kwa upande wa Pemba na Unguja ambao watachuana hadi fainali,”.

“Tukumbuke kuwa kombe hili la Karume Cup linafanyika chini ya udhamini wa familia ya Rais wa kwanza wa Zanzibar na gemedari wa mapinduzi matukufu ya Zanzibar Sheikh Abeid Amani Karume chini ya uongozi na mdhamini Mkuu Ahmed Karume lengo kuu likiwa ni kumkumbuka na kumuenzi pamoja na kuyaenzi yale yote mazuri aliyoyafanya,” amesema kiongozi huyo.

Katika michuano hiyo kundi A linaundwa na timu za Stone Town, African Magic, Usolo na Millennium huku kudhi B likiundwa na timu za Nyuki, Polisi, JKU na New West zote za wanaume.

Kwa upande wa timu za wanawake zipo JKU, KVZ, KZU na New West ambazo zitacheza kwa mtindo wa Ligi na timu itakayopata alama nyingi ndiyo itakayotwaa ubingwa.

Katika michuano hiyo, inayochezwa kwa upande wa Unguja na Pemba, bingwa kwa upande wa wanawake na wanaume wataondoka na kitita cha Sh. 500,000, kombe, jezi seti moja na mpira mmoja, Sh. 300,000, kombe, jezi seti moja na mpira mmoja itakwenda kwa msindi wa pili kwa upande wa wanawake na wanaume wakati washindi wa tatu wataondoka na Sh. 150,000, mpira na jezi seti moja.