May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Hizi ndizo sababu za watu kuogopa kuoa/kuolewa

Na  Aveline Kitomary,TimesMajira Online,Dar es Salaam

KUMEKUWA  na tatizo la watu hasa vijana  kuogopa kuingia katika mahusiano au ndoa  kutokana na sababu mbalimbali  ikiwemo mitazamo hasi katika jamii.

Woga huo umefanya watu wengi kuchelewa kuoa/kuolewa ingawa  umri unaruhusu kufanya hivyo.

Zipo sababu mbalimbali ambazo zinachangia vijana kuogopa kujiingiza katika mahusiano ya kudumu/ndoa.
 

Mtaalmu wa Saikolojia kutoka Chuo cha Kikatoliki cha Mwenge (MWECAU), Cristian  Bwaya analiambia Jarida la Majira ya Afya kuwa  ni kweli wapo watu ambao wanaogopa mahusiano kutokana na sababu za kisaikojia .

Akizungumzi sababu ya hali hiyo Bwaya anasema yapo mambo mengi yanayoweza kusababisha hali hiyo ikiwemo hofu.

“Kuna mtu anamiaka 30 lakini anaogopa kuanzisha mahusiano ya kudumu  kama ni mwanaume anaona bora awe na mahusiano ya muda mfupi huyo mtu akitaka kuwa serious  anakatisha mahusiano mara moja.

“Wako watu ambao wako tayari kuwa na  mahusiano ya kirafiki lakini sio ya ndoa ila wanataka kuwa katika  mahusiano,”anabainisha Bwaya.

DALILI  ZA ANAYEOGOPA MAHUSIANO/NDOA

Bwaya anasema watu wanaoogopa mahusiano mara nyingi wanategemea kupata mabaya katika mahusiano (hawana imani tena).

“Mtu anategemea mabaya akiwa kwenye mahusiano kuwa lolote linaweza kutokea au  anaweza kuumizwa, utakuta anasema wanaume sio waamini ,nitanyanyasika ,nitakosa uhuru kuwa na mtu ambaye anamchunga.

“Walio wengi wanaogopa akiingia kwenye ndoa anaweza kuumizwa kuwa mwenzake atamsumbua na kuwa wanadoa halali hataki talaka hiyo inamuumiza hivyo anaona bora kuwa kwenye mahusiano kuwa akishindwa anaachana nae.

“Lakini pia sababu muhimu kuna mtu anahofu anajiona mkamilifu sana hivyo anahitaji mtu mkamilifu ,anajiona mzuri sana ,anaweza kuishi maisha yake hivyo akiingia kwenye mahusiano anaona hakuna mtu analingana nae ,”anaeleza Bwaya.

SABABU ZA KUOGOPA

Malezi ni sehemu muhimu zaidi katika kumjengea mtoto uwezo  wa kujiamini hadi pale  anapokuwa mtu mzima.

Kwa mujibu wa Mwanasaikolojia Bwaya, mahusiano mabaya kati ya wazazi yanaweza kuchangia watoto wakikua kujiingiza katika mahusiano ya kimapenzi na hata ndoa.

“Tunajifunza namna ya kupenda kuhusina  na watu kupitia wazazi wetu tunapoona mahusinao yao hayapo sawa kuna mtu anaona baba anamtesa mama mwingine anaona mama anamtesa baba huyo anawaza akiingia kwenye mahusiano anaweza kupata mateso.

“Kuzaliwa katika mazingira ya ugomvi wa baba na mama wakidhalilishana ,kupigana mtoto kama huyu akikua anahitaji msaada wa kisaikolojia ili kuweza kustahimili mahusiano,”anafafanua.

Anasema uzoefu mbaya wa mahusiano kupitia kwenye maumivu ,kuonyeshwa dharau na kukatishwa taama kwa mtu ambaye hujategemea inaweza kuwa na hofu ya kuwa kwenye mahusiano.

“Wapo walioteswa na kuumizwa anaona wanaume wote watakuwa hivyo au wanawake wote wako hivyo,Lingine ni tatizo la kiafya kuwa anashida na hawezi kusema na akiingia kwenye mahusiano shida inaonekana.

“ Inaweza ikawa upungufu fulani ambao utaonekana atakuwa anaogopa kuingia au hata mapungufu ya kimaumbile.

Sababu nyingine anayoiainisha ni kusikia matukio ya usaliti  na maumivu hivyo huwajengoa hofu vijana kuwa wakiingia kwenye anaweza kuwa na wasiwasi.

“Pamoja na kuwa kunashida wapo watu wanaishi vizuri na wamependana kwa muda mrefu.

“Halafu kingine ni ulinzi  kwamba mtu hajiamini ,hajipendi anaona hatakubalika na wengine au huyo mtu anaweza asitoshe kwake.

Kuhusu uhaba wa fedha anasema sio sababu kubwa  katika kuingia kwenye mahusiano au ndoa  

“Lakini hatuwezi kuiacha hili  kwenye suala ya kiuchumi ni kisingizio lakini haina nguvu sana ila ipo.

HII NI MBINU YA KUSHINDA

Bwaya anasema changamoto zote zinatatulika lakini muhimu ni kusamehe na kufungua ukurasa mpya  wa maisha.

Anasema endapo mtu ataamua kuanza maisha upya inaweza kufanya kufanikiwa zaidi katika kila anachokifanya na kuwa mwenye kujiamini na furaha zaidi.

“Kwanza kama kuna tatizo mfano kwa wazazi  tugundue kuwa kama baba na mama wanachangamoto hata wewe hauwezi kuwa hivyo, unatakiwa  uangalie wanakosea wapi na wewe katika mahusiano yako urekebisha hicho ili kuwa salama zaidi.

“Kama unahofu kabla ya kuoa au kuolewa ni bora uombe ushauri ili uweze kusaidiwa na  kama ulikutana na mtu alikunyanyasa haimaanishi wengine wako hivyo ni bora kusamehe na kuanza upya kwasababu ukiliweka sana hilo linaweza kukusumbua.

Msaikolojia Bwaya anasema  ni muhimu unapoingia katika ndoa upate taarifa za kutosha ambazo ni  nzuri za kutia moyo  na matumaini mazuri kuhusu mahusiano na ndoa.

“Sasa vijana wengi  wanaongea mambo mabaya hasa stori za watu waliokosea  katika mahusiano ikiwa ni pamoja na usaliti,ndoa kuvunjika na mengine sasa ukikutana hayo inawajaza hofu hivyo ni vyema wakatafuta taarifa njema kuliko hizi ili wasonge mbele.

“Ushauri wangu kwa Wazazi wajitahidi kulinda watoto katika ugomvi wao ili kuwasaidia watoto wao katika mahusiano na pia kuzungumza mazuri ya watu badala ya mabaya.

“Watu watazame mfano wa wazee walioishi kwenye ndoa muda mrefu itawajengea vijana kujiamini kuingia na kumudu mahusiano yao.

Bwaya anashauri vijana na makanisa kurahisisha mfumo wa ufungaji ndoa bila kuwa na gharama kubwa ya fedha.

“Lakini kuhusu uchumi mfano kanisani kwanini kukiwa na mtu anayependana na mwenzake waoane bila kutumia gharama kubwa.

“Kwasababu wapo Wengi wanaona akitaka kuoa  ni lazima kutumia gharama, kwanini wanawaza ufahari wa gharama za harusi kitu ambacho sio lazima ,nashauri makanisa na nyumba za ibada iwasaidie wanotaka kuanza maisha ya pamoja  waanzishe bila gharama.

“Vijana wasaidiwe unaweza kuanzisha familia bila kuvaa suti na shela inawezekana kutotumia gharama kubwa wakati wa kufunga ndoa na nawashauri vijana wafanye vitu virahisi hii itawasaidia kujenga uimara wa maisha ya ndoa walenge zaidi maisha,”anashauri Msaikolojia.