April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

‘Cheti cha kuzaliwa kina umuhimu kwa mtoto’

MFUMO thabiti wa usajili na vifo ni kichocheo cha ukuaji kwa sekta ya viwanda nchini, hivyo ni wajibu Watanzania kushiriki kikamilifu kampeni inayoendelea ya kusajili watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano.

Ni haki ya mtoto kisheria kutambuliwa,lakini zaidi ya hapo akishatambuliwa, lazima apate nyaraka ya uthibitisho ya kutambuliwa kwake ambayo ni cheti cha kuzaliwa.

Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimabli kwa lengo la kuleta maboresho ya mfumo wa usajili kupitia mkakati wa kitaifa wa usajili matukio muhimu ya binadamu na takwimu.

Cheti cha kuzaliwa ni nyaraka pekee ya utambulisho ambavyo kisheria hutumika kuthibitisha umri wa mtu, mahali alipozaliwa wazazi na taarifa nyingine za mtoto. vilevile hutumia kama kitambulisho, ili kumwezesha mtoto kupata huduma nyingine za msingi.

Baadhi ya huduma hizo nyingine za msingi ni kumwezesha mtoto kupata nafasi ya masomo kwa shule za msingi na sekondari na kuzuia ajira ya watoto.

Zingine ni kuwawezesha wanafunzi kupata nafasi za masomo na mikopo katika vyuo vya elimu ya juu, ni nyaraka ya lazima ili kupata ajira katika taasisi za serikali na majeshi ya ulinzi na usalama na kinamwezesha mtoto kupata haki ya kurithi.

Mwaka 2013 Serikali ilizindua mpango wa usajili wa watoto walio na umri chini ya miaka mitano ambao unaendelea kutekelezwa katika mikoa 15.

Mikoa hiyo ni pamoja na Mwanza, Mbeya, Iringa, Njombe, Songwe, Geita, Shinyanga, Lindi, Mtwara, Simiyu, Mara, Dodoma, Singida pamoja na mikoa ya Morogoro na Pwani.

Hivi karibuni mpango huo ulizinduliwa katika mikoa ya Morogoro na Pwani uzinduzi uliofanyika katika viwanja vya ndege mkoani Morogoro.

Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini (RITA), Profesa Hamis Dihenga, anasema mpango huo ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa usajili wa matukio muhimu ya binadamu na takwimu wenye lengo la kuboresha hali ya usajili wa matukio ya vizazi, vifo, ndoa na talaka.

Takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2012 ilikadiriwa kuwa asilimia 13.4 tu ya wananchi wa Tanzania Bara ndio ambao wamesajiliwa na kupata vyeti vya kuzaliwa.

Anasema kama wakala wamechukua hatua mbalimbali na mpango huo ni moja ya maboresho yanayoendelea kufanyika.

Anasema kupitia mpango huo wanahakikisha watoto wote wanapata vyeti vya kuzaliwa bure na si kubaki na matangazo kama ilivyokuwa awali.

“Vyeti vinajazwa kwa mkono na ni halali kwa matumizi kama vile vinavyochapishwa kwa njia ya mashine. Huduma zinapatikana karibu na maeneo ya wananchi katika ofisi za watendaji kata na katika vituo vya tiba vinavyotoa huduma za afya ya mama na mtoto.

“Matumizi ya teknolojia kwa kutumia simu za kiganjani katika kuchukua na kuzisafirisha taarifa kwenda katika kanzidata ya RITA hivyo,kusaidia utunzaji na upatikanaji wa kumbukumbu kuwa wa ufanisi zaidi,” anasema.

Anasema utekelezaji wa mpango huo katika mikoa iliyotangulia umeonyesha mafanikio na kwamba mpaka sasa zaidi ya zaidi ya watoto milioni 3.6 wamesajiliwa na kupata vyeti vya kuzaliwa na kupandisha wastani wa kitaifa wa watoto waliosajiliwa kutoka asilimia 13 mwaka 2012 na kufikia asilimia 49 mwaka 2019.

“Mpaka sasa mikoa 12 kati ya 13 ambayo mpango huu umeanza kutekelezwa ina wastani wa zaidi ya asilimia 70 ya watoto waliosajiliwa na kupata vyeti vya kuzaliwa. Mikoa mitatu kati ya hiyo ikiwa na wastani wa asilimia 100 na kwa ujumla takwimu hizi zinaonyesha mafanikio ya kiwango cha juu.

“Mikoa ya Morogoro na Pwani haina sura tofauti ya kitakwimu na ile ya wastani wa kitaifa, kabla ya kuanza mpango huo ni watoto asilimia 11 kwa Mkoa wa Morogoro na asilimia 14.5 kwa Mkoa wa Pwani ndio waliokuwa wamesajiliwa,’’anasema Dihenga.

Anasema utekelezaji wa mpango huo katika mikoa ya Morogoro na Pwani unajumuisha matumizi ya vituo vya usajili 716 katika Mkoa wa Morogoro na vituo 513 katika Mkoa wa Pwani na kwamba watoto 560,731 wanategemewa kusajiliwa na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa katika mikoa hiyo.

Anasema watakamilisha awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mpango huo katika mikoa 13 hivyo Morogoro na Pwani ni mikoa ya awamu ya pili huku wakilenga kukamilisha utekelezaji kwa mpango huo katika mikoa iliyobaki ya Tanzania Bara.

Kwa upande wake Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Augustine Mahiga, ameipongeza RITA na wadau wengine kwa kuwezesha watoto zaidi ya milioni 3.6 kusajiliwa.

“Naendelea kufuatilia kwa karibu maendeleo ya usajili katika mikoa hii ya Morogoro na Pwani, naamini hamtaniangusha na kama kuna changamoto tuzibaini, tuzijadili zipatiwe ufumbuzi ili tuweze kusonga mbele,’’anasema Dk. Mahiga.

Hata hivyo anasema elimu kwa uuma bado ni muhimu kwani wananchi wanahitaji kukumbushwa mara kwa mara hivyo uhamasishaji endelevu unatakiwa kufanyika pande zote zinazohusika.

Waziri huyo anasema vyeti vinavyotolewa katika mpango huo vinajazwa kwa mkono kwani si rahisi kupeleka kompyuta katika vituo vyote na lazima ieleweke Tanzania si nchi ya kwanza kufanya hivyo.

“Naomba kama waziri aliye na dhamana na masuala ya usajili kutamka kwamba vyeti vinavyotolewa kwa watoto katika mpango huu ni nyaraka halali ya Serikali na ina thamani sawa katika matumizi kama kile kinachojazwa na mashine.

“Nimesikia kuna baadhi ya taasisi za Serikali zinasita kutumia vyeti hivyo yakiwemo majeshi ya ulinzi na usalama ambao viongozi wake katika ngazi ya mkoa tupo hapa na tumeshiriki katika hatua za awali za maandalizi hivyo, sitegemei hali hii kujitokeza katika mikoa yetu,” anasema Dk. Maiga.

Dk. Maiga amesisitiza uadilifu kwa wasaidizi wanaotoa huduma hizo sambamba na kutaka ieleweke kuwa huduma hiyo ni bure hivyo akawatahadharisha wasaidizi wa usajili wasitumie mpango huo kama fursa ya kujipatia kipato.

Naye Kaimu Kabidhi Wasihi Mkuu wa RITA, Emmy Hudson, anasema kuna umuhimu wa kusajili watoto na matukio mengine kama vifo, ndoa na talaka ili Serikali iwe na takwimu sahihi.

“Tunaposajili vifo pia inakuwa rahisi kwa Serikali kufahamu eneo gani lina tatizo na hata kufahamu idadi ya watu wanaofariki kutokana na maradhi eneo husika,”anasema Emmy.

Tangu kuanzishwa kwa kampeni hiyo katika mikoa 13 tayari watoto 3,778,556 sawa na asilimia 49 wamesajiliwa.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Katiba na Sheria, Mohamed Mchengerwa, ambaye pia ni Mbunge wa Rufiji aliwataka wakazi wa Pwani kujitokeza kwa wingi na kuendelea kuhamasishana siku hadi siku ili watoto waandikishwe kwa wingi.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Regina Chonjo, aliwataka viongozi mbalimbali kujitokeza na kutumia majukwaa yao ya dini na siasa kuhamasisha wazazi kujitokeza ili watoto na vijana waandikishwe kwa wingi.