April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Jamii ina uelewa mdogo juu ya watu wenye ulemavu wa ngozi

Na Mohammed Sharksy (SUZA)

KILA inapofika Juni 13 ya kila mwaka dunia huadhimisha Siku ya Kimataifa ya uelewa wa watu wenye ulemavu wa ngozi yaani (albino).

Dhamira kubwa ni kutambua umuhimu wa kulinda haki za watu wenye ulemavu wa ngozi, wakati huu ambapo wanakumbwa na madhila ikiwemo kuuawa kwa imani za kishirikina.

Imezoeleka sana miongoni mwa wanajamii kusema maneno yanayoonyesha dharau, ubaguzi, unyanyapaa, udhalilishaji na kuondoa utu wao kwa watu wenye ulemavu wa ngozi kwa jamii ya ualbino kama vile mzungu, zeru zeru na kadhalika.

Lakini hali hii ya ualbino ni maumbile yalioenea ulimwenguni kote ambayo inaathiri watu wa aina mbali mbali au jamii zote bila kujali rangi au asili yao.

Mbali na kwamba dunia imeathirika na shida hii ya ualibino lakini Afrika Mashariki inaongoza zaidi kuliko sehemu nyingine za dunia.

Kwa mfano,nchini Tanzania kuna albino mmoja kwa wakazi 1,400, sawa na wastani wa kimataifa ni albino mmoja kwa watu 20,000.

Ualbino hutokana na urithi kutoka kwa wazazi wawili baba na mama, Wazazi wote wawe na ulemavu huo au la watakuwa na jeni za sifa bainishi za albinism kabla ya kuzaliwa kwa mtoto mwenye ualbino.

Tafiti nyingi zimeonyesha kwamba wazazi wote wanapokuwa na tabia bainishi za albinism na hata kama hakuna mzazi aliye na ulemavu huo kuna uwezekano wa moja kati ya nne au asilimia 25 ya kila ujauzito kuwa mtoto atazaliwa na ualbino.

Ualbino ni maumbile ya binadamu ambayo huzaliwa na hali ya kukosa uwezo wa kujenga rangi( pigmen)ya melanini ambayo ni muhimu kama kinga dhidi ya mnururisho wa jua. Watu wenye ualbino huwa na nywele nyeupe au manjano, na ngozi nyeupenyeupe. Macho yao ni bluu au hata pinki.

MTAALAMU WA TIBA YA WATU WENYE UALBINO

Akizungumza na makala haya Dkt.Hafidh Hassan,ambae ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Ngozi katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja, anasema kwamba takwimu zimeonyesha kwamba Zanzibar kuna watu wenye ualibino 186.

Anasema kati ya hao Unguja ni 102 na Pemba ni 84,hata hivyo, anasema kuwa Wanzanzibari wenye ualibino ni waelewa sana kuhusu hali yao ya kimaumbile na kufuata taratibu zote za utunzaji wa mwili kutumia ‘lotion’ na uvaaji wa nguo na miwani kwa ajili ya kujikinga na muuangaza.

Aidha Dkt.Hafidh anasema kuhusu utumiaji wa dawa bado kuna changamoto kama vile mahudhurio madogo miongoni mwa watu kutoka mikoa ya kusini na kaskazini Unguja ambapo huweza kuwasababishia athari kwa miili yao.

“Kumekuwa na ukosefu wa takwimu za watu wenye ualbino kutoka visiwa vyengine kama visiwa vidogovidogo vya Pemba na Tumbatu)”, alisema.

Sambamba na hilo,lakini daktari huyo anasema baadhi ya wazazi na wakezi wenye watoto wenye ualbino,anasema kwamba katika kliniki zote ambazo zipo Unguja na Pemba ni wagonjwa kati ya 60 mpaka 70 tu ndio wanaohudhuria kliniki.

“Kukosekana kwa vifaa kama vile kofia, miwani,dawa za kupaka kwenye mdomo (lip bum ukosefu wa liquid nitrogen ambayo ingesaidia kutibu ngozi zilizogundulika kua na viashiria vya saratani ni moja ya changamoto iliyopo kwa sasa”, anasema.

Hata hivyo,aliipongeza Wizara ya Afya kutokana na jitihada zake za kusaidia baadhi ya vifaa tiba kwa atu wenye ualbino jambo ambalo linawapa faraja kubwa.

Nae mmoja kati ya watu wenye ualibino ambae hakupenda kutajwa jina lake aliiambia makala haya kuwa baadhi ya jamii au watu wamekuwa wakiwaona kwa mtazamo tofauwatu wenye ualbino.

“Baadhi ya sehemu ukipita watu au hata watoto wanakutazama na kukuona tofauti sana jambo ambalo tunajiskia vibaya”, anasema.

Alisema hali hiyo inaendeleza unyanyapaa ka ka jamii na hivyo baadhi ya wenye ualbino hushindwa kujichanganya na watu wengine ka ka jamii na shughuli mbalimbali za kijamii na kitaifa.

ATHARI ZA UALIBINO

Kuna matatizo mengi wanayoweza kuyapata watu wenye ualibino ikiwa ni pamoja na mwendo wa macho wa mara kwa mara, upande mmoja hadi mwingine au kwa kuzungukazunguka (Nystagmus).

Athari nyingine ni kwamba watu wenye ualbino mara nyingi huwa na makengeza yaani kukosa uwiano wa misuli ya macho (Strabismus) makengeza.

Sambamba na hilo, lakini wenye ualbino pia hupatwa na mata zo ya kushindwa kuangalia kwenye mwangaza mkali (photo phobia). Aidha athari nyengine ni pamoja na kupooza kwa macho (esotropia), uwezo mkubwa wa kupata saratani ya ngozi.

Mbali na kwamba tatizo hili la ualibino linaathari nyingi kiafya bado kuna na changamoto nyingi zinazowakumba watu wa aina hii ikiwa ni pamoja na chngamoto za kielimu, hatari ya kutengwa kwa sababu ya maumbile yao.

Pia watu wenye ualbino hupata unyanyapaa wa kijamii hasa ndani ya jamii wanazoishi ambapo ndugu na jamaa baadhi yaw engine huwatenga.

NINI KIFANYIKE ILI KUZIPIGA VITA CHANGAMOTO WANAZOPATA

Familia na skuli hazina budi kufanya juhudi za kuwajumuisha watoto wenye ualibino katika shughuli za vikundi au za pamoja bila kuwabaguwa.

Kutokana na uoni hafifu unaowakabili watu wengi wenye ualibino hawawezi kusoma ubaoni katika hali ya madarasa ya kawaida kwa hiyo basi,walimu hawana budi kufanya juhudi ya ziada kupanga upya darasa ili kuwaweka mbele na karibu zaidi na ubao.

Aidha watu wenye aina nyingi za albinism wanahitaji kuchukua tahadhari kuepuka kuathirika kwa ngozi zao na mionzi ya jua.

Athari za ngozi zinaweza kuepukwa kwa kujipaka mafuta ya kuzuia mionzi ya jua,kuvaa kofia na nguo ndefu za kukinga mionzi ya jua.

Hivyo basi ipo haja ya jamii kuwa na uelewa mpana kwa watu wenye ualbino na kuwaona ni watu wa kawaida ka ka jamii na si kuwanyanyapaa kama ilivyo baadhi ya watu wanavyofanya.