April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCBRT, Jeshi la Polisi kupima wananchi macho bure kesho

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira,Online, Dar

HOSPITALI ya CCBRT kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi nchini kesho wataendesha zoezi la upimaji macho bure kwenye Hospitali ya Polisi iliyopo Barabara ya Kilwa maarufu kama ‘Hospitali ya Polisi Kilwa Road.

Hospitali hiyo ipo katika katika Wilaya ya Temeke mkoani Dar es Salaam. Upimaji macho huo utaenda sambamba na kusherekea Siku ya Macho Duniani.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na CCBRT Jijini Dar es Salaam leo, maandalizi kwa ajili ya zoezi zima la upimaji macho yamekamilika na kutoa wito kwa wananchi wote kujitokeza kwa wingi ili waweze kupima macho.

Aidha, taarifa hiyo imesema kuwa Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Jokate Mwegelo sambamba na Afisa Mtendaji Mkuu wa CCBRT, Brenda Msangi pamoja na maofisa mbalimbali wa Jeshi la Polisi ataongoza zoezi hilo muhimu.

“Upimaji wa macho utakwenda sambamba na upimaji wa miwani kwa wale watakaogundulika kuwa na tatizo la macho,” taarifa hiyo imesema na kuongeza kuwa CCBRT itaendeleo kushirikiana na taasisi mbalimbali za Serikali katika kuwafikia wananchi wengi zaidi hapa nchini.

Hospital ya CCBRT ambayo imejiwekea heshima kubwa hapa nchini kwa kupunguza vifo vya mama na mtoto, imekuwa kinara pia kwa kutoa huduma za macho ikwemo pia utengenezaji wa miwani na huduma zinginezo za afya ya binadamu.

Taarifa ya hospitali hiyo, Siku ya Macho Dunia inachukuliwa kwa umuhimu kwa kipekee kwani jicho ni nyenzo muhimu katika maisha na maendeleo ya binadamu hiovyo Watanzania wajenga tabia ya kupima macho mara kwa mara.

“Tunachukua nafasi kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kuwahamasisha wananchi wa Dar es Salaam kujitokeza kwa wingi kuja kupima afya ya macho kwani huduma hiyo itatolewa bure,” ilisema taarifa hiyo.

Katika Mkutano wa Mwaka wa Mashirika na Taasisi zisizo za Kiserikali (NGOs) uliofanyika Jijini Dodoma na kufungwa na Rais wa Jamhuri wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, Hospitali ya CCBRT ilishinda Tuzo ya utoaji wa huduma bora za afya