May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Zamseed: Wakulima tumieni maonesho ya nanenane kujifunza mbegu bora kuenenda na mabadiliko ya tabianchi

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

Wakulima wametakiwa kutumia maonesho ya nanenane ili kujifunza kilimo cha kisasa pamoja na kutambua mbegu bora ambazo zinaweza kustahimili magonjwa na kuenenda na mabadiliko ya tabianchi.

Hayo yameelezwa na Ofisa Masoko,Bwana Shamba wa kampuni ya uzalishaji wa mbegu za mazao mbalimbali ya Zamseed ya nchini Zambia, Emmanuel Paul,wakati Timesmajira online ilipotembelea banda lao katika maonesho ya nanenane Kanda ya Ziwa Magharibi yanayofanyika katika viwanja vya Nyamh’ongolo wilayani Ilemela mkoani Mwanza.

Emmanuel, ameeleza kuwa wapo kwenye maonesho ya nanenane tangu Agousti 1, mwaka huu Kwa ajili ya kuwaelimisha wakulima Ambapo wamepanda mazao mbalimbali kwa ajili ya kuwafundisha wakulima namna bora ya kulima kisasa na matumizi ya mbegu bora.

Ameeleza kuwa mkulima ili aweze kupata mbegu bora anapaswa kuhudhuria maonesho kama hayo ya nanenane aweze kujifunza na kuangalia mwenyewe kwa sababu mbegu bora haiji kwa maneno bali kwa kuona.

Ambapo ameeleza kuwa mbegu zao zimetengenezwa kwa namna ya kukinzana na magonjwa mbalimbali yanayosababishwa na udongo pia kupambana na wadudu wanaoshambulia mbegu huku wakimshauri mkulima kupulizia dawa kwa kiasi kidogo endapo ataona wadudu wapo kwa asilimia 25.

“Akifika hapa ataona na anaweza kuchagua na kujua mbegu ipi ni bora Zamseed mbegu zetu zinazalishwa nchini Zambia,wakulima wachague mbegu hizi ambazo zinatoa mazao makubwa makubwa na mahindi yake yanatoka watoto wa wawili wawili,zinavumilia ukame,ambapo Kishapu tumelima ambalo ni eneo korofi la ukame lakini mahindi na yamefanya vizuri lyanavumilia magonjwa mbalimbali ata kama yatapita lakini ukifunua kwa ndani bado yamebeba,”ameeleza Paulo.

Pia ameeleza kuwa mwitikio ni mzuri katika banda lao ambapo tangu Agousti 1-4 ,watu takribani 400 wametembelea banda lao huku maswali wanayouliza ni je mbegu inavumilia ukame hivyo inaonekana wakulima changamoto yao ni mvua zimekuwa za wasiwasi.

“Wakulima mambo yamebadilika kuna mazao tulikuwa tunalima bila shida ikiwemo tikiti lakini kwa sasa hali ya hewa imebadilika kuna mazoa bila kutumia mbegu za kisasa ambazo zimetengenezwa kwa namna ya kupingana na magonjwa mbalimbali hayawezi kuwa na tija,njooni mjifunze namna ya kupanda,kulima na kutumia mbegu bora pia mawasiliano ili ukikutana na changamoto tuweze kukushauri,”.

Kwa upande wake mmoja wa wakulima, Steven Shija ameeleza kuwa changamoto ya mabadiliko ya hali ya hewa imesababisha kupata hasara kwani wamevuna tofauti na walichotarajia kutokana na uwekezaji walioufanya.

“Wakulima tubadilike tuchimbe visima tufanye uwekezaji kwenye kilimo cha umwagiliaji, wataalamu waangalie ni aina gani za mbegu zitatufaa katika msimu husika kwa kuzingatia mabadiliko ya tabianchi,mfano mwaka jana tulitumia mbegu tulizozoea mvua ikawa chache,”ameeleza Shija.

Ofisa Masoko,Bwana Shamba wa kampuni ya uzalishaji wa mbegu za mazao mbalimbali ya Zamseed ya nchini Zambia, Emmanuel Paul, akionesha namna kabechi ilivyostawi katika shamba darasa lao lililopo katika viwanja vya Nyamh’ongolo katika maonesho ya nanenane Kanda ya Ziwa Magharibi yanayofanyika katika viwanja hivyo wilayani Ilemela mkoani Mwanza.(Picha na Judith Ferdinand)
Ofisa Masoko,Bwana Shamba wa kampuni ya uzalishaji wa mbegu za mazao mbalimbali ya Zamseed ya nchini Zambia, Emmanuel Paul,akizungumza wakati Timesmajira online ilipotembelea banda lao katika maonesho ya nanenane Kanda ya Ziwa Magharibi yanayofanyika katika viwanja vya Nyamh’ongolo wilayani Ilemela mkoani Mwanza.(Picha na Judith Ferdinand)

Mmoja wa wafanyakazi wa kampeni ya Zamseed, mwenyewe tisheti ya kijani akumuonesha mmoja ya wananchi walipotembelea Banda na shamba darasa lao lililopo katika viwanja vya Nyamh’ongolo wilayani Ilemela kunakofanyika maonesho ya nanenane Kanda ya Ziwa Magharibi.(Picha na Judith Ferdinand)
Baadhi ya wananchi wakiwa katika banda la kampuni ya uzalishaji wa mbegu za mazao mbalimbali Zamseed walipotembelea banda hilo katika maonesho ya nanenane Kanda ya Ziwa Magharibi yanayofanyika katika viwanja vya Nyamh’ongolo wilayani Ilemela mkoani Mwanza.(Picha na Judith Ferdinand)