April 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

RC Chalamila: Ushirikiano ndiyo nguzo ya mafanikio

Na Ashura Jumapili TimesMajira Online, Kagera,

MKUU wa Mkoa wa Kagera, Albert Chalamila,ameomba ushirikiano kutoka kwa viongozi mbalimbali wa serikali na dini wakati wa utekelezaji wa majukumu yake ili waweze kuuinua mkoa huo kiuchumi na kuufanya kuwa eneo la kuvutia uwekezaji.

Chalamila ,ameyasema hayo leo baada ya kukabidhiwa ofisi na aliyekuwa mkuu wa Mkoa huo Meja jenerali Charchel Mbuge katika ukumbi wa mkuu wa mkoa wa Kagera.

Anasema ili Mkoa wa Kagera uwe chachu ya maendeleo na vyema kuwa na ushirikiano wa dhati na mshikamano wenye lengo la kujenga na kuimarisha shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Anasema mambo ya kuzungumza pembeni kuhusu jambo la kujenga taswira nzuri ya mkoa haisaidi hivyo hakuna budi kuzungumza kwa uwazi.

‘’Ndani ya ushirikiano tusipende kuoneana kwenye mambo yasiyokuwa na faida badala yake tujenge umoja thabiti ili tuweze kujenga Kagera yenye manufaa kwa wananchi wake “amesema Chalamila.

Anasema anamshukuru Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kumteua tena kuwa mkuu wa mkoa wa Kagera baada ya likizo fupi.

“Nilipo sasa ni mpya kweli kweli katika kuitumikia serikali yangu,wanasema kila kitu ni makusudi ya mungu”amesema mkuu huyo wa Mkoa.

Anasema amekabidhiwa mkoa wenye Wilaya saba na halmashauri 8,tarafa 27,Kata 192,Vijiji 662,vitongoji zaidi ya 3000 na mitaa 66.

Anasema mkoa una shule za msingi 1030 za serikali zikiwa 938 zenye wanafunzi laki 7 na sekondari 288 za serikali zikiwa 220 zenye wanafunzi laki moja wakati wanafunzi wa kidato cha tano na sita wakiwa 12,000.

Aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Kagera Meja jenerali Charles Mbuge,anasema katika utendaji wake mkoani humo hakujiangusha katika utendaji wake na hakumuangusha rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Samia Hassa aliyemteua Aprili 15,mwaka 2021.

Meja Jenerali Mbuge,anasema yeye ni mkuu wa mkoa wa 24 katika mkoa wa Kagera tangu Tanzania ilipopata uhuru na amekuwa katika nafasi hiyo kwa muda wa mwaka mmoja na siku 13.Amemuambia mkuu wa mkoa mpya kuhakikisha anasimamia miradi yote ya serikali inakamilika kwa wakati na kwa viwango vyenye ubora na thamani ya fedha.

Amemueleza kuweka kipaumbele kwenye majukumu ya kitaifa ikiwemo sensa ya watu na makazi, inayotarajiwa kufanyika Agost 23,mwaka huu ,kilele cha mbio za mwenge wa uhuru mkoani humo kuwa maandalizi ya awali yameshafanyika ,mradi mkubwa wa bomba la mafuta unaotokea nchini Uganda unapita mkoani humo na zao la kahawa ambalo limeanza kuwanufaisha wakulima.

Katibu tawala mkoa wa Kagera (RAS )Toba Nguvila,anasema Meja jenerali Mbuge,alikuwa msaada mkubwa wa wilaya zote za mkoa huo alisimama kama baba.Anasema alikuwa ni mkuu wa mkoa asiyependa majungu na aliyefanya kazi zake kwa weledi na uadilifu mkubwa.

“Mnyonge mnyongeni haki yake mpeni alikuwa ni kiongozi asiyependa miradi ya maendeleo ikwame,aliimarisha ulinzi na usalama mipaka yote ya mkoa na simu yake alipokea namba za watu wote waliompigia bila kujali itikadi zao”anasema Nguvila.

Anasema Meja jenerali Mbunge,ni mtu mwenye upendo wa dhati hakuwa mnafiki ukikosea anakueleza hapo hapo.Mwisho.

Kutoka kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Kagera Albert Chalamila na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa huo Meja jenerali Charles Mbunge wakati wa makabidhiano ya ofisi.