April 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa kanda ya Mbeya Dkt Godlove Mbwanji

Wenye ulemavu wa kusikia wanakabiliwa na changamoto

Na Esther Macha,TimesMajira Online,Mbeya

WATU wenye ulemavu wa kusikia wanakabiliwa na changamoto mbalimbali katika jamii ingawa hazionekani kwa macho na changia jamii kutofahamu changamoto wanazoikabiliwa nazo .

Hayo yamesema juzi na Mwenyekiti wa Chama cha Viziwi Mkoa wa Mbeya(CHAVITA), Tusa Mwalyega wakati akizungumza na mwandishi wa habari hizi kuhusiana huduma ya kitengo cha mkalimani kwa Viziwi katika hospitali ya Rufaa ya Kanda.

Aidha Mwalyega amesema kwamba Hospitali ya Rufaa Mbeya imekuwa ya kwanza kuweka huduma ya mkalimani kwa ajili ya viziwi.

“Hili ni jambo jema kwetu sisi kwani hivi sasa tutaweza kutibiwa vizuri uwepo wa mkalimani huyu ni msaada mkubwa kwetu “amesema Mwenyekiti huyo.

Hata hivyo amesema kuwa uwepo was mkalimani utaboresha utoaji wa huduma kwa kundi hilo ambalo limekuwa likikumbana na changamoto nyingi katika kupata huduma katika sekta ya afya.

Akizungumza kupitia mkalimani wa lugha za alama Faraja Mbwilo, Mwenyekiti wa Chavita amesema kuwa Hospitali imetoa nafasi ya kuwepo kwa mkalimani lakini hiyo ni fursa kwa viziwi kujiendeleza kielimu ili waweze kuajiriwa katika sekta mbalimbali ikiwamo afya na kuwasaidia wenzao ambao huwa wanashindwa kupata huduma kwa sababu tu ya tatizo la mawasiliano.

“Leo asubuhi wakati tunafika tulikuwa wengi mlinzi wa hospitali akatuzuia tusiingie akidai muda wa kuona wagonjwa bado, hata nilipojaribu kuongea nae na kumueleza sisi ni viziwi hakuamini hadi nilipomfuata Mkurugenzi wa hospitali ya Kanda Dkt.Godlove Mbwanji ndipo tukaruhusiwa kuingia”amesema.

Amesema kuwa ulemavu wao umekuwa una changamoto nyingi kwa jamii kwakuwa hauonekani kwa macho.

Kwa upande wake Katibu wa Chavita,Queen Majembe amesema kitendo kilichofanywa na Hospitali ya Rufaa Kanda ni hatua kubwa katika kukabiliana na changamoto za kimawasiliano kati ya watoa huduma za afya na viziwi ambapo alisema hatua hiyo itafungua milango kwa taasisi nyingine za umma na binafsi.

Akizungumza uwepo wa kitengo hicho mkurugenzi wa hospitali ya rufaa ya Kanda ya Mbeya Dkt.Godlove Mbwanji alisena uwepo wa kitengo hicho utakuwa msaada mkubwa wakati wa kupata matibabu kwa watu wenye ulemavu wa kusikia Viziwi.

Mkazi wa kata ya Iyela Ezekiel Kamanga alisema kuwa kuwepo kwa kitengo cha wakalimani katika hospitali ya Rufaa kutasaidia watu wengi wenye ulemavu wa kusikia Viziwi kujitokeza hospitali kupata matibabu na kutawasaidia kuelewa maradhi ,ushauri wa wataalam na maelekezo ya matumizi ya dawa.

“Changamoto hii imekuwa kubwa hususani katika janga hili la Corona kwani wengi wao hushindwa kupata elimu inayotolewa na wataalam na hivyo watu hao wanaweza kusambaza maradhi bila kujijua”amesema Kamanga.

Mwisho.