April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Vyama vya ushirika vyaipa tano benki ya kilimo

Na Mwandishi Wetu, Tabora

VYAMA vya Msingi vya Ushiriki vimeipongeza Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) kwa kuviwezesha mikopo inayofikia zaidi ya sh. bilioni 160, sambamba na kuchochea kasi ya ukuaji ya sekta ya kilimo nchini.

TADB kama mdau muhimu wa kimkakati kwa vyama vya ushirika , imetoa mikopo inayofika 127,606,775,585 kwa vyama vya ushirika na 22,030,864,870 kwa Vyama vya Msingi vya Kilimo na Masoko (AMCOS), ambapo 10,964,000,000 zimetolewa na benki hiyo kupitia Mfuko wa Dhamana kwa Wakulima Wadogo (SCGS).

Kwa mujibu wa taarifa ya TADB, jumla ya vyama vya ushirika saba na AMCOS 141 ndizo zimeshanufaika na mikopo hiyo na kuwawezesha wakulima kwenye maeneo mbalimbali nchini kukuza na kuendeleza shughuli zao za kilimo.

Akizungumza mjini hapa katika sherehe za kuazimisha Siku ya Ushirika Duniani Mwenyekiti wa Chama cha Ushirika cha Msingi Chato (CCU), Deogratius Didi amesema TADB imerejesha heshima ya wakulima wa zao la pamba wilayani kwake na maeneo mengine Kanda ya Ziwa.

“Tangu Benki ya Kilimo ianzishwe hapa nchini, maisha ya wakulima wa pamba yamebadilika kwani wamekuwa na uhakika wa pembejeo na soko la kuunzia pamba,” amesema na kuongeza kuwa CCU, imeweza kununua pamba kutoka kwa mkulima kwa bei nzuri.

Didi amesema mbali ya kuipongeza TADB kwa kuvijengea uwezo vyama vya ushirika ameshuruku Serikali ya Awamu ya sita chini Rais, Samia Suluhu Hassan kwa kuwahakikishia wakulima, wafugaji na wavuvi kuwa itaendelea kuiongezea mtaji benki hiyo ili iweze kutoa mikopo mingi zaidi na yenye riba nafuu.

“Uhai na ustawi wa CCU, umetokana na mkopo tuliopata TADB. Benki ya Maendeleo ya Kilimo kwetu sisi wakulima wa pamba ni mkombozi,” amesema na kuongeza kuwa vyama vya ushirika na AMCOS kupitia mikopo ya benki, vipo katika nafasi nzuri ya kuchangia mapinduzi ya kilimo.

TADB imechangia kuleta mageuzi makubwa kwenye mazao kahawa, pamba na uvuvi kwa Kanda ya Ziwa kilimo cha mpunga, ufugaji wa ng’ombe wa maziwa na mkonge kwa Kanda ya Mashariki, kilimo cha mahindi kwa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, kilimo cha alizeti kwa Kanda ya Kati na kilimo cha ufuta Tunduru mkoani Ruvuma.

ends………….