April 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri Bashungwa aagiza vituo vya huduma kwa Mteja kila Mkoa

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Innocent Bashungwa amemuagiza Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI Prof. Riziki Shemdoe kuweka mikakati ya uanzishwaji wa Kituo cha kutolea huduma kwa mteja kwa kila Mkoa ili kurahisisha utoaji wa Huduma bora kwa wananchi.

Ametoa agizo hilo leo wakati alipotembelea Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Ofisi ya Rais –TAMISEMI kwa lengo la kuangalia maelekezo aliyoyatoa kuhusu maboresho ya kuhakikisha huduma bora inatolewa kwa wananchi.

“Nimeridhishwa na utendaji kazi wa watumishi wa Kituo cha Kutolea Huduma kwa Wateja cha Ofisi ya Rais –TAMISEMI lakini ingekuwa vyema vituo hivyo vingekuwa vinapatikana katika ngazi ya Mikoa ili kuwarahisishia wananchi kupata huduma kwa haraka tofauti na sasa mpaka wapige simu Wizarani kutatuliwa kero zao, hivyo tunawajibu wa kuweka mikakati ya kushusha huduma hizo mikoani kuwapunguzia adha wananchi kufuata huduma ngazi ya Wizara” Amesisitiza Waziri Bashungwa

Amemuagiza katibu Mkuu huyo kuhakikisha anatafuta rasilimali fedha na vifaa ili kuhakikisha ule makakati wa kuweka nguvu na kuimarisha Sekretarieti za Mikoa katika utoaji wa huduma bora kwa wananchi kuanzia ngazi ya kijiji, kata, Tarafa , Wilaya na Mkoa unafanikiwa.

Ameagiza kuwa Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala wa Mikoa ndio watakaokuwa wasimamizi wakuu wa vituo hivyo vya kutolea Huduma kwa wateja lengo likiwa ni kuhakikisha huduma bora inapelekwa kwa wananchi kwenye maeneo yao na kuwapunguzia adha ya kutembea umbali mrefu kufuata huduma Wiazarani.

“Jambo hili limeanza vizuri ngazi ya Wizara, hivyo tuimarishe kwenye Mikoa ili kuweza kuwasaidia wananchi, hivyo nawaagiza kuhakikisha tunaweka mikakati ya kila Mkoa kuwa na Kituo cha Huduma kwa wateja ili wananchi wanapohitaji huduma kutoka Mikoani wanakuwa na namba ambazo wanaweza kupiga badala ya kutoka Vijijini kuja kupata huduma Wizarani.” Amesisitiza Waziri Bashungwa

Naye Msimamizi wa Kituo cha Huduma kwa Wateja Antelma Mtemahanji amesema kuwa lengo la kuanzishwa kwa kituo hicho ni kuwasaidia wananchi waliokuwa wakitembea umbali mrefu kutoka vijijini hadi kufika Ofisi ya Rais –TAMISEMI kufuata huduma mbalimbali za kiofisi na toka kituo kimeanzishwa mwaka 2020 hadi sasa simu 125, 381 zilizopokelewa na kufanyiwa kazi katika kituo hicho.

Aidha , amesema kabla ya kuanzishwa kwa kituo hicho Ofisi ya Rais –TAMISEMI ilikuwa ikipokea wateja 100 hadi 120 ambao walikuwa wakifika ofisini kufuata huduma, lakini hali hiyo kwa sasa imepungua na kupunguza mlundikano wa wananchi kufuata huduma Wizarani