May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watano mbaroni tuhuma za kufanya njama za kuiba mabomba mradi wa maji Buswelu

Judith Ferdinand, Timesmajira Online, Mwanza

Watu watano wanashikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza kwa tuhuma za kufanya njama za kuiba mabomba ya mradi wa maji Buswelu mali ya Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA).

Akizungumzia tukio hilo kwa waandishi wa habari mkoani hapa Aprili 24,2024 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Wilbroad Mutafungwa, ameeleza kuwa Aprili 22 mwaka huu majira ya saa 3 usiku maeneo ya Nyamadoke Kata ya Kahama wilayani Ilemela jeshi hilo lilipokea taarifa kutoka kwa raia wema kuwa katika eneo hilo kwenye mradi wa maji Buswelu, Kahama na Nyamadoke, kuna watu wanaiba mabomba ya mradi huo kwa kuyapakia kwenye gari.

Baada ya ufuatiliaji wa haraka jeshi hilo lilifanikiwa kuwakamata watu watano
ambao ni Iddy Hamis kwa jina maarufu Nduta, (30) fundi bomba na mkazi wa Isamilo wilaya ya Nyamagana,Method Charles kwa jina maarufu Anthony (44), fundi bomba na mkazi wa mtaa wa Ndofe Kata ya Igoma Wilaya ya
Nyamagana.

Huku wengine ni Mikweba Irangi kwa jina maarufu Mibaya (53) mkazi wa
Buzuruga Wilaya ya Ilemela,Fredy Nyakega (46) dereva na mkazi wa Nyasaka Wilaya ya Ilemela na Salumu Husein kwa jina maarufu Pembe (32)
dereva wa MWAUWASA na mkazi wa Nyasaka “A” Wilaya ya Ilemela wakiwa wanakimbia ili wasikamatwe kuhusiana na wizi wa mabomba 30 yenye thamani ya milioni15.96 ambayo
waliyapakia kwenye gari lenye namba za usajili T.551 EDM aina ya FAW ikiwa na “tela’
lenye namba za usajiliT.897 ECW.

“Upelelezi wa tukio hili unaendelea na mara utakapo kamilika, wahusika wote
watafikishwa mahakamani, jeshi linatoa wito kwa wananchi kuendelea kulinda miradi yote inayotekelezwa na serikali isihujumiwe kwa kutoa taarifa za uahalifu na wahalifu ili ziweze kufanyiwa kazi kwa haraka na miradi yote iendelee kubaki salama,”ameeleza Mutafugwa –