May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

PPRA yasaini mkataba wa makubaliano wa shilingi bilion 40

Na Mwandishi wetu Dodoma.

MAMLAKA ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA),imesaini mkataba wa makubaliano wa shilingi bilion 40,  na  Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP),kwa ajili ya kusaidiana katika maeneo matatu .Maeneo hayo makubwa matatu ni pamoja na kuwajengea uwezo katika Ununuzi wa Umma, kuwajengea uwezo wadau wakiwemo wakandarasi na eneo la tatu ni kuwezesha mamalaka hiyo kupata vitendea kazi.Akizungumza leo Aprili 24, 2024 jijini Dodoma  mara baada ya kusaini mkataba huo Mkurugenzi Mkuu wa PPRA, Eliakim Maswi amesema Mamlaka hiyo imeingia mkataba huo ili kuwezeshwa kuwa na vitendea kazi.Maswi  ameeleza PPRA inashughulika na ukaguzi wa thamani hali ya fedha zinazotumika katika nchi na kwamba hawawezi kupewa vifaa kabla hawajasaini mkataba.Ameongeza kuwa makubaliano hayo walianza kujadili mwaka 2022 ambapo yalipita katika Wizara ya Fedha na Tume ya mipango na baadae yakakubalika kwa ajili ya kusaidiana. Amesema kuwa UNDP ni ya ulimwengu hivyo kutokana na kufanya manunuzi makubwa katika ulimwengu ni vizuri  nao wakasaidia ili kujiimarisha katika eneo la kujenga taasisi na uwezo wa watu ambao wanahusika na Ununuzi wa Umma.Sheria yao ya Ununuzi wa Umma ilipitisha mwaka jana moja ya eneo ambalo walijadili na wabunge ni kuwezesha wazawa kutumika kusimamia miradi mikubwa nchini huku akisema sheria hiyo inasema miradi yote ambayo ni chini ya bilioni 50 lazima iwe ya wazawa.“Kama kuna mradi wenye ukubwa zaidi ya hiyo lazima kampuni itakayosimamia, kuongeza lazima iwe ya wazawa pia ili kampuni za wageni zihamishe utaalum walionao kuja kwa wazawa hivyo UNDP wamekubali kutujengea uwezo wakandarasi wetu wadogo ili waweze kuwa na uwezo wa kufanya kazi vizuri, “amesema.

 “Tunamshukuru Rais wetu Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kutuwezesha kujenga jengo letu na sasa tunamiliki jengo hili tofauti na awali tulikuwa tumepanga,” amesema Mkurugenzi huyo.Naye Mtaalam wa Miradi ya maendeleo ya UNDP, Deogratias Mkembela amesema kuwa mkataba huo na makubaliano yanawapa fursa zaidi ya kuwa na mashirikiano na PPRA pamoja na kuwarahisishia ufanyai kazi na mamlaka hiyo.Ameongeza kuwa makubaliano hayo yameainisha maeneo kadhaa wa kadha ya kuisaidia serikali nakwamba wanatarajia kuwawezesha, kuwafikia vijana, wanawake na makundi maluum.