May 2, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watakiwa kuachana na imani potofu ya kupata tiba ya chanjo ya UVIKO-19

Na Judith Ferdinand,TimesMajira Online Mwanza

WANANCHI wametakiwa kuachana na imani potofu pamoja na kuachana na dhana ya kwenda kwa waganga wa kienyeji kupata tiba ya UVIKO- 19.

Kwani hawatapata msaada wowote wa tiba bali kinga bora na salama ya UVIKO-19 ni kupata chanjo ya ugonjwa huo.

Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel kwa wananchi wa kata ya Maligisu Kijiji cha Kadashi na waliokuwa katika viwanja vya Kwideco wilayani Kwimba mkoani hapa.

Hiyo ikiwa ni muendelezo wa kuwapatia uwelewa juu ya ugonjwa huo na umuhimu wa kuchanja kuwa ni njia moja wapo ya kujikinga na maambukizi ya UVIKO-19.

Mhandisi Robert, amesema kila mwananchi lazima awe na ndoto ya maisha ya baadae,hivyo elimu sahihi ya chanjo inahitajika ili wawe salama.

Amesema wananchi wanapaswa watambue kuwa chanjo ni salama na wajifunze kufuatilia maelekezo yanayotolewa na wataalamu wa afya na waachane na imani potofu waangalie usalama wa afya zao.

” Elimu potofu zimekuwa nyingi tumepoteza wafanyakazi wetu kwa ugonjwa huu ni hatari, tusidanganyike kwa sababu miruzi mingi humpoteza mbwa mwelekeo hivyo tuchanje ili kuokoa maisha na kuwa na afya bora, ukweli nilipata hofu pale ambapo tulijikuta kila mtu ni msemaji wa chanjo kwenye mitandao hii ni hatari sana,”amesema Mhandisi Robert.

Kwa upande wake Mwenyekiti Mwenza wa Kamati ya Amani Mkoa wa Mwanza Askofu Charles Sekelwa,ametoa wito kwa watanzania kuepukana na maneno ya mitandao yasiyo na ukweli bali wajikite katika uzalendo na upendo wa nchi yao.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel Akizungumza na wananchi wa kata ya Maligisu Kijiji cha Kadashi na waliokuwa katika viwanja vya Kwideco wilayani Kwimba mkoani hapa, ikiwa ni muendelezo wa kuwapatia uwelewa juu ya ugonjwa huo na umuhimu wa kuchanja kuwa ni njia moja wapo ya kujikinga na maambukizi ya UVIKO-19.Picha na Judith Ferdinand

Amesema,viongozi wa dini zote wana umoja na ushirikiano katika kupambana na ugonjwa huo,hivyo wananchi wachangamkie fursa hiyo ili kujenga afya na kuendelea kasi ya uchapaji kazii ili kujijenga kiuchumi nakukuza maendeleo binafsi na taifa.

“Chanjo ni salama wananchi wajitokeze kuchanja ili kuleta amani na muungano wa kifamilia na taifa,nimesimama hapa Kwimba kama shahidi mtumishi wa Mungu kuwaombeni wanakwimba tujiepusheni na propaganda zisizo za kweli,” amesema Askofu Sekelwa.

Mmoja wa wananchi wa Wilaya ya Kwimba Lucas Machibya,amesema wameguswa na kuamua kuchanja kwa sababu chanjo ni salama hivyo waliishukuru serikali kwa kuwaletea chanjo ambayo inanusuru maisha ya watanzania huku wakieleza kuwa imani ya kutokuchanja inaenezwa na watu wachache ambao siyo wakweli .

” Nimehamasika mwanzo niliogopa baada ya kusikia maneno waliokuwa wanasema ukichanja damu itaganda lakini nashangaa kuona ndugu zangu waliochanja wapo vizuri na hawakupata madhara yoyote na leo Mkuu wa Mkoa ametuhakikiahia amechanja na mimi leo nimechanja na nipo salama,”amesema.