March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wataka ubunifu kuwa njia ya kuleta maendeleo

Na David John,TimesMajira Online,Dar

WADAU wanaohusika na masuala ya ubunifu wamekutana jijini Dar es Salaam kupitia Kongamano maalum la wabunifu ambalo limeandaliwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia(COSTECH).

Washiriki wa kongamano la ubunifu wakiwa katika kongamano hilo

Katika kongamano hilo limefanyika jana, ambapo wadau hao wameelezea kuhusu hatua zinazochukuliwa wabunifu kwa kushirikiana na wadau wengine kuhakikisha ubunifu unakuwa njia mojawapo ya kuleta maendeleo.

Akizungumza wakati wa kongamano hilo Mkurugenzi wa Tafiti, Sera na Mipango katika Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Alfred Mkombo amewaeleza wabunifu na wadau hao kuwa kazi yao ni kusimamia masoko ya mitaji kuhakikisha biashara zinazohitaji mitaji zinapata kupitia utaratibu uliopo.

Mkurugenzi Mkuu Kampuni ya Phema Agri Daniela Kwayu(katikati) akitoa mchango kuhusu ambavyo wamekuwa wakisaidia wakulima katika masuala mbalimbali yanayohusu kilimo na teknolojia

“Leo tumekuwa na warsha ya kuangalia ubunifu katika maeneo ya biashara zinazoanza na biashara za kati kwamba namna gani hizi biashara zinapata mitaji kupitia masoko ya mitaji na sisi kama Mamlaka ya Masoko na mitaji tunasaidia ubunifu katika masoko ya mitaji.

“Mojawapo ya jukumu la mamlaka ni kuendeleza masoko ya mitaji na ili kuendeleza ni lazima usimamie ubunifu, biashara ya ubunifu na ubunifu katika bidhaa na huduma zinazohitajika kwa wananchi.

“Kwa hiyo sisi tunawachagiza wananchi hasa vijana wawe wabunifu zaidi.Sasa hivi tuna mpango ambao tunafanya kwa ushirikiano na UNDP katika kutengeneza miongozo ya kusimamia mipango ya mitaji shirikishi.Tunaposema mitaji shirikishi ni utaratibu wa kupata fedha kwa ajili ya kuendeleza mradi fulani unapata fedha,”amesema.

Sehemu ya wadau wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kumaliza kwa kipindi cha kwanza cha Kongamano maalum la majadiliano kuhusu sekta ya ubunifu na wabunifu.Kongamano hilo limefanyika jana jijini Dar es Salaam na limeandaliwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kwa kushirkiana na COSTECH pamoja na UNDP kupitia Programu yake ya Ubunifu –Funguo na mdhamini Mkuu ni Kampuni ya Simu ya Voda-Tanzania

Amefafanua mtu anachanga fedha kidogo kidogo kama inavyofanyika msibani au kwenye makanisa lakini ile fedha sasa wanaichukua na wanaipeleka kwenye uzalishaji.

“Ukusanyaji huu unakuwa tofauti kidoogo kwasababu unakusanywa kupitia mitandao au majukwaa ya mitatandao ya kieletroniki na hii mitandao ni lazima iwe imesajiliwa , kwa hiyo tunafanya huo mpango , tunaandaa miongozo kwa ajili ya uendeshaji” amesema.

Akifafanua kuhusu kongamano hilo amesema kumekuwepo na wabunifu mbalimbali na mipango mbalimbali ya ubunifu imeangaliwa na kujadiliwa kwa kina.Kwa hiyo ametoa rai kwa Watanzania kuchangamkia fursa zinazotokana na ubunifu.

Kwa upande wake Ofisa kutoka COSTECH Promise Mwakale amesema wameshiriki kongamano hilo la wabunifu kama wadau katika kufunga masoko kwa ajili ya ubunifu.

“COSTECH imekuwa ikitoa ruzuku kwa ajili ya wabunifu na tunatoa ruzuku kuanzia kwenye mawazo na kuwakuza ,kwa hiyo kongamano hili ni muhimu kwetu kwani limejumuisha wadau wengine katika kufungua masoko na kuongeza mitaji kwa ajili ya wabunifu”amesema Mwakale.

Aidha Mtalaamu wa Fedha kutoka UNCDF Paul Damocha amesema wao mbali ya kuwa moja ya wadhamini katika Wiki ya Ubunifu wamekuwa wakishiri katika kukuza na kuendeleza ubunifu kwa njia tofauti kwa kushirikiana na COSETCH, Serikali na wadau.

Pia wamekuwa wakisaisia katika sekta ya fedha, sera na kutengeneza miongozo pamoja na kuelekeza idara za Serikali katika kutengeneza mazingira wezeshi kwa wabunifu na kuwapatia leseni.

“Kumekuwa na jitihada kubwa za kitalaam za kusaidia wajasiriamali kuanzisha biashara zao, mambo ya teklonojia na biashara.Kuhusu ubunifu tunaona haja ya kushirikisha washika dau wengi pamoja na mashirikia makubwa kama UNDP, Idara ya Habari na Mawasiliano,” amesema

Sehemu ya washiriki wakifuatilia mijadala , maoni na michango kuhusu bunifu na wabunifu nchini hasa katika kuangalia mbinu mbalimbali ambazo zitasaidia kuendeleza wabunifu na kada nyingine za aina hiyo

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu Kampuni ya Phema Agri Daniela Kwayu amesema wao wamejikita katika kutumia teknolojia mbalimbali kuwasaidia wakulima pamoja na kuwawezesha katika pembejeo.

Kuhusu ushiriki wao kwenye Kongamano la Ubunifu Kwayu amesema wao ni miongoni mwa kampuni ambazo zimepata msaada mkubwa kutoka CMSA na hivyo wameshiriki ili kutoa ushuhuda wa am ambavyo wamefanikiwa na sasa wanasaidia wakulima wengi nchini.

Ametoa rai kwa vijana wa Tanzania kuhakikisha wanatumia vema uwepo wa teknolojia kwa kubuni masuala mbalimbali yanayoweza kuwaingizia kipato badala ya kutumia muda mwingi kwenye mitandao kufanya yasiyokuwa na tija.