May 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wanaojifanya madalali nyumba Mradi Magomeni Kota waonywa

Na Mwandishi wetu Timesmajira online Dar

MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Amos Makalla ametembelea mradi wa nyumba za magomeni kota ambapo na kutoa onyo kali kwa watu wanaojifanya ni madalali wa kuwatafutia watu vyumba katika mradi huo jambo ambalo ni kinyume na taratibu.

Makalla ametoa onyo hilo Mkoani Dar es Salaam alipofanya ziara ya kutembelea mradi huo ambao unasimamiwa na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA).

Amesema Serikali itawachukulia hatua kwa wote watakaobainika kujihusisha na utapeli huo, huku akiagiza vyombo vya ulinzi na usalama kuwasaka matapeli hao na kuwataka wakazi nwa kaya hizo 644 kupuuza maneno yanayotolewa kuwa nyumba hizo zinapangishwa.

“Nimetembelea mradi huu leo nimeona hakuna wapangaji wapya na vyumba havina watu,hakuna sehemu ya kupangisha zaidi ya wakazi wa kaya 644 wa magomeni kota ambazo ndizo zinazopaswa kukaa katika majengo haya”amesema Makalla.

Aidha, ameiomba menejimenti ya Wakala wa Majengo TBA,kutumia maeneo ambayo yamebaki kimkakati na kufanya mambo mengine makubwa, Mkoa wa Dar es Salaam ardhi ni shida hivyo wanapaswa kuitumia kimkati.

Hata hivyo,amesema Watanzania wanapaswa kuwa makini na watu wanaojifanya madalali kwa ajili ya kupangisha nyumba hizo, na kuwataka kutowasikiliza matapeli hao .

Kwa upande wake Kaimu Mtendaji wa TBA, Said Mdeme amesema mradi huo kwa sasa umekamilika kwa asilimia 99 na kinachoendelea kwa sasa ni zoezi la ufungaji trasfoma kwa ajili ya umeme pamoja na lifti.

Mdeme amesema kabla ya wakazi hao kuingia katika vyumba hizo, TBA itatoa semina elekezi juu ya namna ya kuishi katika majengo hayo.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Amos Makalla akisisitiza jambo wakati akizungumza na Mkuu wa wilaya kinondoni Godwin Gondwe (Kushoto) na pamoja na Kaimu Mtendaji TBA,Said Mdame, walipofanya ziara katika Mradi wa Nyumba za Magomeni Kota leo, jijini Dar es Salaam.

“Serikali imetumia gharama nyingi sana kwa ajili ya kutekeleza mradi huu hivyo tunawaomba wakazi wa kaya 644 kulinda eneo hili,”amesema Mdeme

Hata hivyo amesema TBA ilipokea maombi zaidi 2,000 kutoka kwa watu ambao walikuwa wanataka kuishi katika nyumba hizo.

Aidha amesema mradi huo umelenga zaidi kaya 644 zilizokuwa zikiishi katika eneo hilo na si watu wengine.

Mwisho