April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ukusanyaji damu wabadilisha mwelekeo

Na Mwandishi Wetu,timesmajira,online

MPANGO wa Taifa wa Damu Salama umebadilisha mwelekeo wake wa kuigeukia jamii ili kukusanya damu kwa ajiri ya kukabiliana na changamoto ya kutegemea wanafunzi wa shule za sekondari iliokuwa ikiwatumia wakati wote.

Akizungumza kwenye uzinduzi wa Kampeni ya Taifa ya Ukusanyaji Damu iliyoanza Septemba 20, 2021, Mkuu wa Idara ya Ukusanyaji Damu katika Mpango wa Taifa wa Damu Salama, Dk. Avelina Mgasa amesema kauli mbiu ya kampeni za mwaka huu ni Changia Damu Kuokoa Wanaoleta Uhai Duniani.
Dk. Mgasa amesema hivi sasa wanaweka mkazo kwa jamii kujitolea damu kwa hiari kwani Mpango wa Taifa wa Damu Salama haujaweza kufikia lengo la kukusanya chupa za damu zinazokithi mahitaji ya nchi.
Ripoti ya Mpango wa Taifa wa Damu Salama imeonesha kwa kipindi cha mwaka 2019/2020 kwa kushirikiana na timu za halmashauri wameweza kukusanya chupa za damu 312,714 zilikusanywa ambazo ni sawa na asilimia 57 ya mahitaji, amesema.
Dk. Mgasa amesema shirika la afya Dunniani (WHO) linaelekeza kila nchi mwanachama kukusanya damu asilimia moja ya wakazi wake au chupa 10 kwa kila wananchi 1,000 ili kujitosheleza na mahitaji ya damu salama wakati wote.
Mkuu wa Idara ya Ukusanyaji Damu katika Mpango wa Taifa wa Damu Salama, amesema kwa takwimu za mwaka 2019/2020 Tanzania tumefikia chupa 6 kwa kila wananchi 1,000.
Akizungumzia changamoto za kupata wachangiaji wa damu, amezitaja kuwa ni pamoja na wanafunzi wanaosoma na hata wanaomaliza shule za sekondari kuwa na umri mdogo kwani sharia inawataka watu wenye umri wa miaka 18 hadi 65.
Asilimia 80 ya damu inayokusanywa nchini inakusanywa kutoka kwa wanafunzi na vijana wanapokuwa shule za sekondari na vyuoni ambao wanamaliza wakiwa na umri mdogo hivyo hawapati fursa ya kuchangia damu wakiwa shuleni na wakirudi kwenye jamii huacha kuchangia, anasema.
Mwisho.