April 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Shirika la WoteSawa lapokea malalamiko ya ‘Housegirl’ kunyimwa mishahara

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online,Mwanza

IMEELEZWA kuwa miongoni mwa changamoto walizokutana nazo mabinti wafanyakazi wa nyumbani kipindi cha mlipuko wa kwanza wa COVID-19,ni pamoja na kufanyiwa vitendo vya ukatili ikiwemo kupigwa na kuachishwa kazi ghafla.

Serikali ilifunga shule na vyuo mara baada ya Covid-19 kuingia nchini hapa Machi 2020, huku baadhi ya mashirika yakisitisha shughuli na wengine kulazimika kufanya shughuli wakiwa nyumbani,hali ambayo ilikuwa changamoto kwa wasichana wafanyakazi wa nyumbani kutokana na kukutana na ukatili zaidi ikiwemo ongezeko la kazi nyingi.

Akizungumza na Majira kwa njia ya simu Ofisa Msimamizi wa Makao na Uwezeshaji wa Shirika la WoteSawa lililopo mkoani Mwanza,Demitila Faustine, amesema katika janga hilo,walikuwa wanapokea kesi nyingi za wasichana wa nyumbani kutokulipwa mishahara na wengine walikuwa wanafanyiwa ukatili.

“Miongoni mwa changamoto katika janga like,ni kazi nyingi, kugombezwa, vipigo, kuachishwa kazi ghafla anaambiwa nenda nyumbani huku anadai mshahara,kunyimwa mishahara na wakati mwingine ukatili wa kingono kwa sababu muda mwingi familia ili kuwa nyumbani na baadhi walilazimika kufanya kazi wakiwa nyumbani huku shule na vyuo vikiwa vimefungwa hivyo kufanya wanaume na vijana katika familia husika wasio waaminifu kutumia fursa hiyo kuwafanyia mabinti ukatili wa kingono,”alisema Demitila.

Amesema,shirika la WoteSawa katika kuhakikisha kipindi hicho cha Covid-19, wasichana wafanyakazi wa nyumbani hawafanyiwi ukatili waliweka mabango mbalimbali ambayo yalikuwa na ujumbe kuwa mfanyakazi salama,familia salama.

“Alindwe na asifanyiwe ukatili kipindi hicho cha COVID-19, lakini pia tulikuwa tunatoa elimu kuwa sasa hivi familia wengi wapo nyumbani na tunawaelimisha jamii kuwa hata kama kuna janga la corona lakini,tunajua mna presha ya kuachishwa kazi pamoja na changamoto lakini wawajibike katika nafasi zao wasiwafanyie ukatili mabinti wa kazi,”amesema Demitila.

Pia amesema,kutokana na elimu waliokuwa wanaitoa kwa kiasi chake imesadia,kesi zilivyopungua tukachukulia kuwa watu wameelewa namna ya kuwalinda wasichana wafanyakazi wa nyumbani.

Sanjari na hayo, amesema walikuwa wanatoa elimu na kuwapatia vifaa vya kujikinga kwa mabinti wafanyakazi wa nyumbani waliokuwa wanashinda nyumbani na wale wa mama ambao wanafanya kazi kwa siku ikiwemo barakoa,vitakasa mikono,sabuni na ndoo kwa ajili ya maji tiririka.

Ofisa Msimamizi wa Makao na Uwezeshaji wa Shirika la WoteSawa Demitila Faustine,akitoa mafunzo ya namna ya kupinga ukatili kwa wafanyakazi wa nyumbani.Picha na Judith Ferdinand

Ambapo walitoa vifaa hivyo vya kujikinga na Covid-19 kwenye kata 10 za Wilaya ya Nyamagana ikiweno Mkolani,Luchelele na Buhongwa.

Hata hivyo amesema, waliendelea kutoa elimu sokoni na stendi kwa kuwaelimisha wananchi kuwa wanapojilinda wenyewe wasisahau kuwalinda wafanyakazi wa nyumbani, kwani asipo mlinda mfanyakazi wa nyumbani moja kwa moja na familia yake yote ipo katika hatari.

Kwa upande wake Mratibu wa shirika la Tanzania Child Domestic Workers Coulition(TCDWC),George Leonard, amesema ,miongoni mwa kesi walizozipokea ni pamoja na kunyimwa mshahara licha ya kuwa midogo ambapo unakuta binti kafanya kazi kwa mwaka mmoja au miwili lakini stahiki zake ajalipwa na akijaribu kudai anabambikiwa kesi, hivyo mambo yanakuwa magumu zaidi upande wao.