May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Shaka: Anayedhani awamu ya sita kutakuwa na mianya ya kufuja fedha anajidanganya

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online, Manyara

KATIBU wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Shaka Hamdu Shaka, amesema iwapo kuna mtu anadhani katika utawala wa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia kutakuwa na mlango wa kufanya ubadhirifu na kufuja fedha za umma, huyo atakuwa anajidanga.

Shaka ameyasema hayo jana alipotembelea utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi kuhusu ujenzi wa miundombinu katika Shule ya Sekondari Ayalagaya Dreda wilayani Hanang’ mkoani Manyara.

“Nataka kuwaambia wanaodhani kuna mlango wa upigaji wa fedha za umma nataka kuwaambia kwamba hayo ni mawazo potofu na dhaifu mno, serikali ya Rais Samia iko makini na inafuatilia mienendo ya fedha hizo zinazotumika. Rais ameteua wasaidizi ambao moja ya jukumu lao la msingi ni kuhakikisha wanaishi na kufanyia kazi maono na dira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.” amesema.

Amesema chini ya Rais Samia, fedha nyingi za miradi ya maendeleo imeshuka mpaka ngazi za chini na matunda ya fedha hizo yanayonekana, hivyo ni wajibu wa kila mtu kuhakikisha fedha inayotolewa kwa ajili ya maendeleo inafanya kazi iliyokusudiwa kwa maslahi ya wananchi na kwamba haitarajiwi kuona zinatumika kinyume na mlango.

Amesisitiza Chama Cha Mapinduzi hakitasita kutoa ushauri kwa serikali kuchukua hatua dhidi ya yeyote ambaye atabainika kufuja fedha zinazotolewa na Rais Samia ambaye ana dhamira ya dhati ya kuwatumikia Watanzania katika kuwaletea maendeleo.

“Hapa Mkoa wa Manyara kuna miradi mingi imetekelezwa na taarifa zilizopo fedha zimetumika vizuri na hiki ndicho tunachotaka kusikia,” alisema.