May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Samia aisuka upya Ikulu, TISS

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

RAIS Samia Suluhu Hassan amefanya uteuzi wa viongozi wanne akiwemo Said Hussein Nassoro kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Usalama wa Taifa (TISS) akichukua nafasi ya Kamishna Diwani Athuman.

Awali, Nassoro alikuwa naibu mkurugenzi mkuu na mkurugenzi wa shughuli za ndani wa idara hiyo.

Katika mabadiliko hayo aliyoyatangaza usiku, Januari 3, 2023, Rais Samia amemteua Diwani kuwa Katibu Mkuu-Ikulu akichukua nafasi ya Moses Kusiluka ambaye ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu KiongoziDiwani ambaye ni Kamishana wa Jeshi la Polisi, amehudumu nafasi hiyo kwa zaidi ya miaka mitatu tangu alipoteuliwa na Rais wa wakati huo, Hayati John Magufuli Septemba 12, mwaka 2019.

Alishika nafasi hiyo kutoka kwa Dkt. Modestus Kipilimba ambaye kwa sasa ni Balozi wa Tanzania nchini Namibia.

Kabla ya Diwani kushika wadhifa huo wa Mkurugenzi wa Idara ya Usalama wa Taifa alikuwa mkurugenzi mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).

Aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Hussein Kattanga ameteuliwa kwenda New York nchini Marekani kuwa Mwakilishi wa Kudumu katika Umoja wa Mataifa (UN).