April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

P.Diddy ashusha tuhuma nzito kwa wazungu

NEW YORK, Marekani

KUFUATIA kuenguliwa kwa mwanariadha Sha’Carri Richardson kwenye mbio za Mita 100, michuano ya Olimpiki 2020 ambayo itaanza Julai 23, mwaka huu huko Tokyo, Japan kwa kile kinachodaiwa mwanadada huyo kutumia Bangi, Rapa mahiri nchini Marekani Seab Love Comb maarufu kama ‘P. Diddy’ameshusha tuhuma nzito dhidi ya wazungu.

Sha’Carri, mwenye umri wa miaka 21 raia wa Marekani, alienguliwa baada ya kufanyiwa vipimo na kubainika kuwa anatumia bangi jambo ambalo limemuudhi sana P.Diddy,

P.Diddy amesema anakerwa na watu mbalimbali hasa wazungu ambao wamekuwa wakimnanga Sha’Carri mitandaoni akiwemo mwandishi mmoja kutoka Australia ambaye alikwenda mbali zaidi na kudai mwanadada huyo ni feki kama zilivyo nywele na kucha zake.

Akizungumza kwa hasira kupitia kwenye ukurasa wake wa Instagram, P. Diddy anawalaumu wote wanaomnanga mwanadada huyo na kusema kuwa bangi haimfanyi mtu awe na mbio zaidi kama baadhi ya watu wanavyodhani kuwa mwanadada huyo amekuwa akishinda kutokana na kutumia kilevi hicho.

Diddy amesema, amechoka kuwaona wazungu wanakaa na kutunga sheria ngumu ambazo ni kwa ajili ya kuharibu na kudidimiza ndoto na malengo ya mtu mweusi, wakiwachukulia kama watumwa.