April 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mkurugenzi wa NEC, Wilson Mahera

NEC yatupilia mbali mapingamizi ya Lissu

Na Joyce Kasiki,TimesMajira Online, Dodoma

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetupilia mbali mapingamizi mawili yaliyowekwa na mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu dhidi ya wagombea wa nafasi hiyo Dkt. John Magufuli wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Profesa Ibrahim Lipumba wa Chaman cha Wananchi (CUF).

Mkurugenzi wa Uchaguzi, Wilson Mahera akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani)

Awali akizungumza na waaandishi wa habari katoka ofisi ya CHADEMA jijini Dodoma kuhusu mapingamizi hayo, Lissu amesema ameweka mapingamizi mawili dhidi ya Rais Magufuli na pingamizi moja dhidi ya Profesa Lipumba kwa madai kwamba hawajakidhi masharti na sheria za uchaguzi.

Lissu alitaja pingamizi la kwanza linalomuhusu Dkt.Magufuli na Profesa Lipumba kuwa ni kupeleka fomu za wadhamini kukaguliwa na kuhakikiwa na wakurugenzi wa uchaguzi na kisha kugongwa mihuri wakati wenye mamlaka ya kufanya hivyo ni NEC kwa mujibu wa sheria za Tume hiyo.

Pingamizi la pili linamuhusu Dkt.Magufuli peke yake ambalo alidai picha zilizoambatanishwa kwenye fomu zake siyo zilizohitajika kwa mujibu wa sheria za Tume ya Uchaguzi ambazo ni picha mdogo (paspot size) lakini mgombea huyo amesema picha zilizopigwa upande na kwamba kinachoonekana ni nusu sura.

“Sababu za kuweka mapingamizi ambayo kwa maoni yangu kwa Dkt .John Magufuli na moja kwa Profesa Lipumba,pingamizi la kwanza ni mgombea kupitisha fomu zake za kutafuta wadhamini kuhakikiwa na kugongwa mihuri na wasimamizi wa uchaguzi wa majimbo,ambao aliwateua yeye na pingamizi hilo pia linamuhusu Profesa Lipumba, huku akisema ni kinyume cha sheria ya uchaguzi,” amesema Lissu.

Lissu amesema NEC ndiyo yenye mamlaka ya kuhakiki wadhamini wote kutoka mikoa 10 ya Tanzania Bara na mikoa miwili Tanzania Visiwani.

Kufuatia mapingamizi hayo Lissu ameiomba NEC baada ya kuwapa muda wa kujitetea waliowekewa mapingamizi na iwakutanishe alioweka na waliowekewa mapingamizi kwa mujibu wa sheria.

Akitoa uamuzi wa NEC, Mkurugenzi wa Uchaguzi, Wilson Mahera amesema kuwa NEC kwa kuzingatia masharti ya kanuni 39(5) ya kanuni za Uchaguzi wa Rais na Wabunge za mwaka 2020, baada kupokea mapingamizi dhidi ya wagombea hao, iliwataarifu mapema iwezekanavyo na wahusika wamewasilisha utetezi wao kwa Tume hiyo.

Akizungumza mapingamizi dhidi ya Dkt. Magufuli, Lissu amesema kwamba hakuambatisha picha kwenye fomu za uteuzi na hakurudisha fomu ya utetezi kwa mujibu wa masharti yaliyowekwa na sheria, Dkt. Mahera amesema “Tume baada ya kupitia sababu za mapingamizi imejiridhisha kuwa Dkt.Magufuli amerejesha fomu zake ambazo zimeambatishwa pamoja na picha kwa mujibu wa sheria ,kanuni na maelekezo ya Tume .

“Hivyo imehiridhisha kwamba mapingamizi hayo hayana msingi wa kisheria na kuyatupilia mbali na kwa maana hiyo Dkt.Magufuli ni mgombea halali wa kati cha rais kupitia CCM,” amesema Mahera.

Kuhusu mgombea wa CUF Dkt.Maheta alisema kwa mujibu wa masharti yaliyowekwa na sheria,Tume baada ya kupitia sababu ya pingamizi pamoja na utetezi uliotolewa ,imehiridhisha kuwa mgombea huyo kupitia Chama cha wananchi (CUF),amerejesha fomu zake kwa mujibu wa sheria ,kanuni na maelekezo ya NEC.

“Hivyo NEC imejiridhisha kwamba pingamizi hilo halina msingi wa kisheria na imelitupilia mbali na kwa hiyo Profesa Ibrahim Lipumba wanaendelea kuwa mgombea halali wa kati cha rais kupitia Chama cha wananchi (CUF).

Aidha alisema kwa mujibu wa kanuni ya 39(6) ya kanuni za uchaguzi wa Rais na Wabunge za mwaka 2020 ,sababu za uamuzi huo wa Tume watapewa kwa maandishi.