May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mo Dewji: Siondoki Simba, sitakubali kukatishwa tamaa

Na Mwandishi Wetu, TimeMajira Online

MWENYEKITI wa Bodi ya Wakurugenzi ya Klabu ya Simba, Mohammed Dewji (Mo Dewji) amesema hatoondoka ndani ya klabu hiyo hadi pale wanachama watakapomtaka kufanya hivyo na wala hatokubali watu wachache hawawezi kumkatisha tamaa ya kutekeleza mipango aliyojiwekea kwa ajili ya kuifikisha klabu hiyo kwenye mafanikio ya juu na kuwa klabu bora barani Afrika.

Mo Dewji ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari kuhusiana na masuala mbalimbali yanayohusu klabu hiyo ambayo imefanikiwa kutwaa kombe la Ligi Kuu Tanzania Bara (VPL) kwa msimu wa tatu mfululizo, Kombe la Shirikisho la Azam (Azam Sports Federation Cup).

Pia msimu huu timu hiyo imeanza vizuri baada ya kutwaa Ngao ya Jamii kwa msimu wa nne mfululizo na kuweka rekodi ya kutwaa kombe hilo mara nyingi zaidi ikiwa ni mara sita.

Kauli hiyo huenda ikawa ni yakuwatoa wasiwasi wanachama na mashabiki wa klabu hiyo kutokana na sintofahamu ya iliyotokea siku chache zilizopita katika mitandao ya kijamii.

Hivi karibuni kuliibuka mjadala ambao ulianzishwa na moja wa wapenzi wa klabu hiyo Dkt. Hamis Kigwangalla ambaye alihoji namna Simba chini ya Mo Dewji walivyompata CEO, Barbara Gonzalez.

Majibizano hayo yalifika mbali hadi kufikia hatua ya Dkt. Kingwangala kuhoji zilipo bilioni 20 za uwekezaji hukupia akiweka wazi kuwa, Mo amemtumia ujumbe na kutishia kutaka kujiondoa kwenye uwekezaji wa klabu hiyo.

Lakini kutokana na kauli hiyo, Mwenyekiti huyo alimtaka Kingwangala kutafuta mahojiano yale aliyofa nya mara ya mwisho na kituo cha redio cha Wasafi ili kutapa majibu na alichoeleza juu ya fedha hizo.

“Watu wachache hawawezi kunikatisha tamaa ya kutekeleza mikakati yangu ya kuifikisha mbali klabu ya Simba. Nitaendelea kubaki Simba hadi wana Simba watakaponitaka niondoke,” amesema Mo Dewji.

Akizungumzia mikakati mbalimbali na hatua ambazo zimekuwa zikichukuliwa kwa ajili ya kuhakikisha Simba inakuwa klabu tishio barani Afrika, Mo amesema katika kipindi cha miaka mitatu bajeti uendeshaji ya timu hiyo imeongezeka kwa asilimia 100.

Amefafanua kuwa, kila mwaka bajeti ya klabu hiyo imekuwa ikiongezeka kwa ajili ya kufanikisha shughuli mbalimbali za uendeshaji wa kalbu ikiwemo usajili wa wachezaji wenye viwango vikubwa ambao watakuwa msaada mkubwa ndani ya klabu yao katika michuano ya ndani na yake ya kimataifa.

Hivi karibuni viongozi wa klabu hiyo waliweka wazi kuwa msimu huu watahakikisha wanafika tena hatua ya makundi katika michuano ya Ligi Mabingwa Afrika au hata zaidi ya hapo.

Kwa mujibu wa Mo Dewji amesema kuwa, kuna mipango ya kuanzishwa Ligi ya Mabingwa Barani Afrika itakayohusisha timu 20 na kwamba mipango hiyo ikikamilika sharti mojawapo linaweza kuwa ili klabu ishiriki mashindano hayo lazima iwe na uwekezaji wa kiasi kadhaa.

“Kutokana na hilo, Simba itahitaji kushiriki mashindano hayo, hivyo ni lazima ikidhi masharti yatatayotakiwa,” amesema Mo Dewji.