April 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mnyama Simba bado yupo mawindoni

Na Iddy Lugendo

KLABU ya Simba imeendelea kumfukuza mwizi kimya kimya huku ikiwa na matumaini makubwa kuwa bado wanauwezo wa kutetea ubingwa baada ya ushindi dhidi ya Coastal Union katika mchezo wa ligi kuu ya NBC uliyochezwa uwanja wa mkwakwani Tanga na kumalizikia kwa Simba kuibuka na ushindi wa bao 2-1.

Licha ya Simba kuanza na mabadiliko machache katika kikosi chao tofauti na wale waliocheza mchezo wa kombe la shirikisho Afrika dhidi ya Gendermerie, ambao hawakuwepo katika mchezo huo na jana dhidi ya Coastal Union walianza kikosi cha kwanza ni Thadeo Lwanga, Pascal Wawa, Clatous Chama.

Mabadiliko hayo ya kocha mkuu wa Simba Pablo Franco katika kikosi cha kwanza bado timu yake ikawa na kikosi bora kwa kilichocheza mchezo wa kombe la shirikisho Afrika mpaka mchezo unaenda mapumziko klabu ya simba ilikuwa mbele kwa bao 1 la Benard Morrison lilifungwa dakika ya 40.

kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku watoto wa Juma Mgunda Coastal Union wakiwa wanalisakama lango la Simba, wahenga walisema ”mgaagaa na upwa hali wali mkavu” ndivyo Coastal Union walichokifanya mbele ya mabeki wa simba na kumuacha Manula akiwa haamini kilichotokea dakika 77 ya mchezo Akpan anaachia mkwaju mkali na kuukwamisha nyavuni.

baada ya Coastal Union kusawazisha bao hilo ikiwa ni kama mnyama simba alikuwa ameshikwa masharubu yake akarudi mchezoni na kuanza kulishambulia lango la vijana wa mkwakani mnamo dakika ya 93 maneno ya wahenga yanatimia kuwa ”ukimuona simba ameloa usidhani ni nyani” katika muda wa jioni mshambuliaji hatari Meddie Kagere anaiweka simba kifua mbele.

Aidha, mpaka mchezo unamalizika katika uwanja wa mkwakwani mkoani Tanga mnyama anafanikiwa kuondoka na pointi tatu muhimu katika mchezo huo ambazo zinawafanya kupunguza pengo lililopo kati yao na vinara wa ligi kuu ya NBC klabu ya Yanga wenye pointi 51 huku simba nafasi ya pili akiwa na pointi 40 na mchezo mmoja mkononi.

kwa upande wake kocha msaidizi wa simba suleiman matola alisema kuwa ”tuliwafunga bao wakasawazisha cha muhimu kilikuwa ni pointi tatu na ndicho tulichofanikiwa dhidi ya wapinzani wetu Coastal Union” sasa Simba wanajianda na mchezo ujao dhidi ya Polisi Tanzania atakaochezwa katika uwanja wa ushirika moshi.

Hivyo Wanalunyasi wanaendelea kumfukuza mwizi kimya kimya huku wakiamini bado ipo nafasi ya kutetea ubingwa wa NBC huku wakiwa nyuma kwa ponti 11 dhidi ya vinara Yanga, Simba inahitaji pointi tatu za mchezo unafuata dhidi ya Polisi tanzania ili kupunguza pengo la pointi 11.