April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kampeni ya ‘Jaza kibubu Na NBC’ kuziona ‘Live’ Simba, Yanga

Na Jackline Martin

BENKI ya Taifa ya Biashara NBC, imezindua Kampeni ya ‘Jaza Kibubu na NBC’ yenye lengo la kuweza kutoa elimu kwa watanzania wote kuhusu utunzaji fedha katika sehemu salama.

Kampeni hiyo itamnufaisha mtumiaji wa Account ya NBC kwenda kushiriki kutazama ‘Live’ kombe la Dunia nchini Qatar na Mechi dhidi ya Simba na Yanga uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam itakayofanyika Aprili 30 mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam leo, wakati wa uzinduzi wa Kampeni hiyo , Mkuu wa Kitengo cha Mauzo na Masoko Abel Kaseko alisema mteja atakayehitaji kushiriki Kampeni hiyo atembelee tawi la NBC au Wakala yeyote akiwa na kitambulisho Cha NIDA ambapo mteja atafunguliwa account na kuongeza kuwa Kampeni hiyo itakuwa na zawadi mbalimbali ambazo zitamfanya mteja kwenda kushuhudia mechi ndani na nje ya nchi;

“Kampeni hii ya ‘jaza kibubu na NBC’ itakuwa na zawadi ambazo zitawawezesha wapenzi wa Mpira kuweza kuhudhuria mechi ya Simba na yanga ambayo itafanyika tarehe 30/4/2022, sisi kama NBC tutagharamikia safari, malazi, chakula na vinywaji kwa watu 50 kutoka mikoani na wapenzi wa mpira waliopo Dar es salaam, tutawazawadia watu 50 pia kuhudhuria mechi hiyo na wote watapewa tiketi ya VIP.

Aidha, Abel alisema mbali na Mechi ya Simba na Yanga kutakuwa na mashindano ya kombe la Dunia ambayo yatafanyika nchini Qatar ambapo wao kama Benki ya NBC watagharamikia vitu mbalimbali kwa mteja ambaye atajishindia kwenda kushiriki kutazama mechi hiyo;

“Tunatambua kuwa mwaka huu kutakua na mashindano ya kombe la Dunia ambayo yanafanyika Qatar mwezi November Hadi Desemba 2022, sisi kama Benki ya NBC tutatoa tiketi 5 kwa watanzania ambao ni wapenzi wa mpira kwenda kushuhudia kombe la Dunia na tiketi zote ambazo tutatoa ni VIP.

“Tutagharamikia pia, safari kwa watu wote kutoka Dar es Salaam hadi Qatar kama malazi, chakula na vinywaji lakini pia tutatoa posho kwa watu ambao wataenda kuhudhuria mechi hizo ambazo ni tiketi za VIP,” alisema Abel.

Mbali na hivyo, Mkuu huyo wa Kitengo cha Mauzo na Masoko alisema Kampeni hiyo iliyozinduliwa jana itaendeshwa ndani ya miezi Sita na mshindi wa kwenda Qatar atapatikana mwezi September 2022.

Naye Meneja Mauzo na Biashara upande wa Wateja Binafsi, Dorothea Mabonye alifafanua Jinsi ya mteja atakavyoweza kujishindia safari ya kwena Qatar, mteja anatakiwa kuweka fedha kuanzia Milioni 7;

“Jinsi ya kufanya ili ushinde safari ya Qatar unatakiwa uweke na fedha kuanzia Milioni Saba na kuendelea lakini Milioni Saba hii unaiweka kidogokidogo mpaka mwezi wa Tisa na ndipo utapata nafasi ya kuingia kwenye droo na uwe mmoja ya wale ambao watakaokwenda Qatar kuangalia live kombe la dunia,” alisema.

Aliongeza kuwa kwa mteja ambae ataweka Milioni 10 na kuendelea kidogokidogo atapata nafasi ya kupata tiketi ya VIP, hivyo kutakua na wateja watano ambapo wawili watakua ni wa VIP na watatu watakua wa tiketi za kawaida.

Doroth alisema, wao kama wadhamini Wakuu wa ligi kuu Tanzania Bara hawajaishia tu kuwapeleka watanzaia Qatar kuangalia kombe la Dunia vilevile wanakwenda kuwazawadia watanzania wote au wateja wa NBC ambao wataweka fedha kuanzia tarehe 6 mpaka tarehe 24/4 mwaka huu kwenda kuangalia mechi ya watani wa jadi Simba na Yanga.

Alisema, kutakuwa na jumla ya washindi 80 ambapo washindi 50 watatokea mkoani na 30 watatokea Dar es Salaam ambao wote watagharamikiwa.

“Tutakuwa na washindi 80 kwa ujumla ambapo washindi 50 watatokea mikoani na washindi 30 watatokea hapa Dar es salaam, washindi 50 tutawagharamikia usafiri kutoka walipo hadi kufika Dar es salaam, malazi na chakula na kutoka hotelini mpaka uwanjani kwenda kuangalia mpira, na washindi 30 ambao tutawapata kutoka Dar es salaam tutawapatia tiketi za VIP kuangalia mechi hiyo”

Kampeni hii ya ‘Jaza Kibubu na NBC’ ni maalum kwaajili ya watenja wa NBC, Wateja binafsi na watanzania wote ambao wangependa kufungua account ya NBC

%%%%%%%%%%%%%%%%%%

Sekta ya Utamaduni, sanaa, michezo zapiga hatua