May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Milioni 5 kusaidia michezo Itenka

Na George Mwigulu, Timesmajira Online,Nsimbo

Timu za mpira wa miguu za shule za msingi na sekondari Kata ya Itenka Halmashauri ya Nsimbo wilayani Mpanda mkoani Katavi zimepatiwa vifaa vya michezo vyenye thamani ya milioni 5 kwa ajili ya kukuza sekta hiyo.

Mbunge wa Jimbo la Nsimbo,Anna Lupembe akitoa vifaa hivyo vya michezo February 21 mwaka huu katika viwanja vya shule ya msigi Itenka wakati wa mkutano wa hadhara amesema kuwa michezo ni muhimu kwenye kutengeneza fursa mpya za ajira nchini.

Lupembe ameeleza kuwa ili vijana waweze kuwa na ushiriki mzuri kwenye sekta ya michezo viongozi wanapaswa kuandaa mazingira mazuri.

Ameeleza kuwa michezo imekuwa kipaumbele chake kwa kuwa husaidia kukuza vipaji kwa vijana wadogo wenye ndoto kubwa za kuchezea klabu pendwa hapa nchini za Simba na Yanga na wakati mwingine malengo yao ni kucheza nje ya nchi.

Kwa kuwa michezo sio tu inajenga afya bali ni chanzo kikubwa cha ajira kwa vijana na kusaidia vijana kujiepusha na makundi ya kihalifu.

Aidha amehimiza vijana kujiunga kwenye klabu za mpira wa miguu kwa kuwa hivi karibuni kuna mashindano yatafanyika ya Lupembe Cup na zawadi zitatolewa.

Mbunge huyo ameeleza zawadi za mashindano yajayo ya mpira wa miguu Jimbo la Nsimbo (Lupembe Cup) amesema kuwa mshindi wa kwanza atapatiwa kiasi cha milioni 2 na kombe,mshindi wa pili milioni 1.5 na kombe,mshindi wa tatu milioni 1,mshindi wa nne 700,000 na mshindi tano,sita,saba na nane kila mmoja atapata kiasi cha shilinhi 100,000 hivyo kufanya jumla ya milioni 5.6 kutumika kutoa hamasa kwenye sekta ya michezo.

Mratibu wa michezo Lupembe Cup jimbo la Nsimbo, Mwl Sayi Elias Mashima amesema kwenye mashindano hayo yanatarajiwa kufanyika Aprili Mosi mwaka huu katika Kata 15 za kimichezo zinazojumlisha jumla ya timu 182 za jimboni humo.

Mashima amesema kuwa mashindano hayo kwa mwaka huu yatakuwa na kauli mbiu ya “ Vijana kushiriki uchaguzi wa serikali za mitaa kwa amani” tafasiri yake yamebeba dhamana ya kuhamasisha vijana kujitokeza kugombea nafasi za uongozi kwa kuwa wanahaki kikatiba ya kuchagua na kuchaguliwa kuwa viongozi.

Amesisitiza kuwa suala la usimamizi bora kwa mashindano hayo ni kipaumbele kikubwa ili kuondoa malalamiko ya klabu zinazoshiriki mashindano ya Lupembe Cup.