May 10, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mgunda awageuzia silaha Maafande wa Ruvu

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

KOCHA mkuu wa timu ya Coastal Union, Juma Mgunda amesema baada ya vijana wake kupata ushindi wa goli 1-0 katika mchezo wao wa ugenini dhidi ya Biashara United sasa wanawageukia Maafande wa Ruvu Shooting watakaokutana nao Aprili 17 katika Uwanja wa Mkwakwani.

Katika mchezo huo wa ugenini Coastal walifanikiwa kupata goli lililofungwa dakika ya 75 na Issa Abushehe na kuwa timu ya tatu kuondoka na alama zote tatu katika uwanja wa Kumbukumbu ya Karume Mara.

Ushindi huo umewafanya Coastal kupanda hadi nafasi ya 13 baada ya kufikisha pointi 30 walizopata baada ya kushinda mechi saba, sare tisa na kupoteza mechi tisa lakini wakiruhusu nyavu zao kutikiswa mara 32 na wao kufunga goli 17.

Kocha Mgunda ameuambia Mtandao huu kuwa, sasa mipango yao wanaihamishia katika mchezo wao wa nyumbani dhidi ya Ruvu Shooting kwani wanachokitaka ni kulipa kisasi kwa Ruvu ambao Novemba Mosi waliwafunda goli 3-1 katika uwanja wao wa Mabatini, Pwani.

Katika mchezo huo, Coastal walikuwa wa kwanza kupata goli la kwanza dakika ya pili ya mchezo huo lililofungwa na Raizin Hafidh lakini Ruvu walisawazisha kupitia kwa Mohammed Banka dakika ya 15 huku magoli yao mengine yakifungwa na Fully Maganga dakika ya 40 na Eradius Emmanuel dakika ya 81.

Mgunda amesema, kilichowapa ushindi katika mchezo dhidi ya Biashara ni marekebisho waliyoyafanya hivyo wanarudi nyumbani hataka kufanya maandalizi ili kuhakikisha wanafanikiwa kulipa kisasi kwa Ruvu na kubakiza alama zote tatu nyumbani.

Pia atahakikisha nyota wake wanacheza na nidhamu na utulivi mkubwa ili kutimiza mipango yao kwani wanatambua uwezo wa wapinzani wao na ili washinde basi ni lazima waoneshe utulivu na kujiamini pia ili kuweza kuzuia kila hatari ya wapinzani wao.

“Licha ya kushinda mchezo wetu lakini bado vijana wangu walifanya makosa kadhaa ambayo tunahitaji kuyafanyia kazi ili kuwa bora zaidi katika uwanja wetu wa nyumbani na kuendeleza furaha ya mashabiki wetu,” amesema Mgunda.