April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mbarali yajipanga kupambana na COVID-19

Na Esther Macha, Mbarali

KAMATI ya Usalama ya Wilaya ya Mbarali ikiongozwa na Mkuu wa Wilaya, Reuben Mfune imeridhishwa na maandalizi yaliyofanywa na ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali kwa ajili ya kuwapokea wahisiwa pamoja na wagonjwa wa Corona (COVID 19) watakaothibithishwa na Wizara ya Afya kama vipimo vitaonyesha wana maambukizi ya ugonjwa huo .

Hayo yamesemwa juzi wakati mkuu huyo wa wilaya alipotembelea kuangalia jengo liloandaliwa kwa ajili washukiwa wa maambukizi ya virusi vya Corona  ambalo lipo kitongoji cha mpunga Relini ambako inajengwa hospitali mpya ya wilaya. 

Aidha Mfune alimtaka Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali kuendelea kufanya maboresho madogo magogo kama usafi wa mazingira ili eneo hilo liendelee kuwa katika hali ya usafi.

“Vitu vilivyobaki ni vidogo sana ila kila kitu kipo tayari hivyo nimwagize Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri vitu vilivyobaki viboreshwe mapema na jengo kukaa katika hali ya usafi”alisema Mkuu huyo wa Wilaya.

Pia Mkuu huyo wa Wilaya alimwagiza Katibu Tawala  pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wawe wanapita mara kwa mara eneo hilo ajili ya kujiridhisha na kuendelea kuboresha mazingira haya hasa suala la usafi.

Alisema wajibu wao mkubwa ni kuhakikisha wanawasimamia mafundi ili kazi ndogondogo zinazoendelea ziweze kukamilika kabisa na elimu ya kujikinga na ugonjwa huo iendelee kutolewa kwa wananchi kwa sehemu zote muhimu.