May 12, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kitita kipya cha NHIF na safari ya Watanzania kufaidi uwekezaji mkubwa wa Rais Samia sekta ya afya

Na Mwandishi Wetu,Timesmajira online,Dar

KITITA kipya cha mafao kwa wanufaika wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) utekelezaji wake unaanza rasmi kesho, huku kikisheheni maboresho ambayo yatanufaisha wanachama wa mfuko huo na watoa huduma.

Aidha, Mfuko huo umewahahakikishia wanachama wake kwamba hakuna mwanachama atakayekosa huduma na umeagiza viongozi na mameneja ya mikoa kutoka ofisini kwenda kujionea hali ya utoaji huduma kuanza kesho kinapoanza kitumika kitita hicho.

Kuanza kutumika kwa Kitita hicho kesho kumetangazwa na Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Bernard Konga, wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, huku akianisha maboresho mbalimbali yaliyofanyika kupitia Kitita hicho.

Amesema Kitita cha mafao ni orodha ya huduma za matibabu ambazo zinatolewa kwa wanufaika wa NHIF na bei zake ambazo hutumika wakati wa malipo kwa madai ya watoa huduma za matibabu.

Amesema mapitio ya Kitita cha Mafao yamefanyika kwa lengo la kuhakikisha kinaendana na mabadiliko pamoja na maboresho mbalimbali yaliyofanyika katika sekta ya Afya chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.

Amefafanua kwamba maboresho ya kitita cha mafao yanalenga kuboresha upatikanaji wa huduma bora kwa wanachama ikiwa ni pamoja na kuongeza huduma ambazo hazikuwepo awali.

Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Bernard Konga

Aidha, Konga alisema yamelenga kufanya maboresho ya huduma na gharama zake kwa kuzingatia maendeleo ya teknolojia na hali halisi ya bei katika soko.

” Nyingine ni kuwianisha Kitita cha Mafao na miongozo ya tiba iliyoboreshwa ili kuongeza ubora wa huduma zinazotolewa kwa wanufaika wa Mfuko,” amesema Konga.

Konga ametaja maeneo yaliyofanyiwa mapitio na maboresho katika Kitita cha mafao kuwa ni pamoja na huduma za usajili na kupata ushauri wa daktari.

Huduma za usajili na kupata ushauri wa daktari

Katika eneo hilo, amesema hatua hiyo inalenga kuwezesha madaktari katika ngazi zote kuwepo kwa uswa wa ada kwa madaktari wa kada zinazoendana .

“Hii itawezesha wanachama kupata huduma za kibingwa katika ngazi mbalimbali za vituo kwa kuzingatia uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika sekta ya afya,”alisema Konga.

Huduma za dawa

Ametaja eneo lingine lililofanywa maboresho kuwa ni la huduma za dawa. Kwa mujibu wa konga jumla ya dawa 736 zimefanyiwa mapitio kwa kuzingatia bei ya soko na gharama za uendeshaji na wastani wa faida.

Amesema hiyo itaondoa changamoto za wanacama kukosa baadhi ya huduma za dawa kutokana na changamoto za bei.

Aidha, Konga amesema kumeongezwa dawa mpya 247 ambazo zinatokana na dawa mpya zilizoko katika mwongozi wa arodha za dawa muhimu za Taifa (NEMLIT) ambapo hatua hiyo imeongeza wigo wa upatikanaji dawa kwa wanachama.

Pia amesema imeingatia mabadiliko katika ngazi ya matumizi ya dawa ama kama zilivyoanishwa katika NEMLIT. “Maboresho haya yataongeza upatikanaji wa huduma za dawa katika vituo vya ngazi ya msingi, mfano dawa za matibabu ya shinikizo la damu na kisuri.

Huduma za upasuaji na vipimo

Eneo jingine lililofanyiwa maboresho ni huduma za upasuaji na vipimo.

Konga amesema gharama za vipimo 311 na huduma za upasuaji imefanyiwa mapitio kwa kuingatia bei bei za soko katika ununuzi wa vifaa na vitendanishi, gharama za uendeshaji na na wastani wa faia hiyo itaondoa changamoto ya kukosekana kwa huduma na vipimo na upasuaji kutokana na changamoto ya bei.

Aidha, amesema maboresho hayo yameongeza wigo wa huduma za kibingwa na ubingwa bobezi za upasuaji na vipimo katika hospitaji za Rufaa ngazi ya Kanda na Taifa.

“Maboresho haya yataongeza upatikanaji wa huduma za matibabu ya saratani, upasuaji wa mifupa, upasuaji wa moyo katika hospitali si za Taifa tu, bali hata hospitali za kanda hivyo kusogeza huduma karibu zaidi na maeneo ya wananchi,” alisema Konga.

Kwa mujibu wa Konga, maboresho ya mwisho ya kitita cha mafao cha NHIF kinachotumika sasa yalifanyika Juni, 2016 takriban miaka nane iliyopita na hivyo kuwepo kwa umuhimu wa kufanya marejeo yake kutokana na sababu mbalimbali.

Ameongeza kwamba katika kuimarisha upatikanaji wa huduma, Mfuko umeendelea kutekeleza, kuimarisha utambuzi wa wanufaika katika vituo vya kutolea huduma kwa kutumia alama za vidole na sura (biometric identifation); ii. Kuweka “platform” mahususi itakayowezesha watoa huduma

kubadilishana taarifa za mgonjwa miongoni mwa vituo; Kuweka utaratibu utakaowezesha wanufaika kuzingatia utaratibu. Kuendelea kudhibiti udanganyifu na kuchukua hatua stahiki kwa wadau watakaodhibitika kujihusisha na vitendo vya udanganyifu.

Amesema Mfuko unaendelea kuthamini na kutambua mchango mkubwa wa wadau wake hasa wanachama na watoa huduma katika kufanikisha utekelezaji wa Kitita hiki kipya.

“Tunaamini maboresho haya yatakwenda kuwa chachu ya kufikia azma ya Serikali ya Afya Bora kwa Wote. Aidha, Mfuko unathamini kazi kubwa inayofanywa na mtoa huduma mmoja mmoja kwa kuzingatia mkataba baina yao na Mfuko, hivyo mawasiliano yataendelea kuimarishwa ikiwemo huduma kwa wateja ili kuwawezesha kufikia malengo yao,” amesema Konga.