May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

JKT yatoa zawadi wodi ya wazazi Chamwino,yafanya usafi

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

JESHI la Kujenga Taifa JKT limeendelea na shughuli mbalimbali katika wiki ya maadhimisho ya miaka 60 ya Jeshi hilo tangu kuanzishwa kwake ambapo limefanya usafi katika kituo cha Afya Halmashauri ya wilaya ya Chamwino pamoja na kutoa zawadi kwa wakina mama waliojifungua kituoni hapo.

Zawadi zilizotolewa kwa akina mama hao ni sabuni ya kufulia pamoja na  pempasi kwa ajili ya watoto waliozaliwa.

Akizungumza mara baada ya kutoa zawadi hizo ,Mkurugenzi wa Ustawi wa Jamii JKT Kanali Regina Matina amesema,katika mwendelezo wa shughuli zinazofanywa na Jeshi hilo  kuelekea miaka 60 ya JKT ,limeona ni jambo la msingi kufanya shughuli hizo kwani nao ni sehemu ya jamii.

“Huu ni mwendelezowa shughuli mbalimbali tunazozifanya  kuelekea miaka 60 ya JKT ,na hapa tumeona ni jambo la msingi kutembelea hospitalini hapa kufanya usafi na kutoa zawadi katika wodi ya wazazi kwani JKT ni sehemu ya jamii ,

“Lakini pia tumeungana na wazazi kama ilivyo majukumu ya JKT ni malezi ya vijana ,uzalishaji mali na ulinzi,na hawa ndiyo wazazi wanaotupatia vijana ,tukaona ni muhimu tusimalize maadhimisho haya bila kuwaona wazazi.”amesema Kanali Matina

Naye Kaimu Mganga Mfawidhi wa kituo cha Afya Halmashauri ya wilaya ya Chamwino John Daniel amelishukuru Jeshi la Kujenga Taifa kwa kuona kituo hicho cha afya kuwa sehemu ya maadhimisho yao ya miaka 60.

“JKT tumekuwa tukishirikiana nao mara nyingi,tumekuwa tukiwaomba msaada mbaimbali na wanatusaidia ,tunaomba waendelee na moyo huo wa kusaidia jamii.”amesema Daniel

Kwa upande wake Arafa Kombe mmoja wa akina mama waliopata zawadi kwa ajili ya watoto wao amelishukuru JKT kwa zawadi hizo na kuliasa liendelee kuwakumbuka wamama huku akilitakia kila la kheri Jeshi hilo katika majukumu yake hususan ya ulinzi wa wa nchi.