April 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

JK:Rais Samia anakwenda vizuri

Na Mwandishi wetu ,timesmajira,Chalinze

RAIS Mstaafu Dk Jakaya Kikwete amesema Rais Samia Suluhu Hassan anaendesha nchi vizuri na kwamba changamoto haziwezi kukosekana.

Dk Kikwete ameyasema haya mbele ya Naibu Waziri wa Afya Dk. Godwin Mollel walipotembelea eneo kutakakojengwa mradi wa jengo la matibabu ya dharura kwenye Hospitali ya Wilaya ya Chalinze iliyopo Msoga mradi huo wa ujenzi unafadhiliwa na ABBOTT FUND ya Marekani kwa gharama ya shilingi Bilioni 1.2 za Kitanzania.

“Tuendelee kumuunga mkono Rais wetu, anayo dhamana kubwa… sio kazi rahisi… ina mawimbi mengi na pengine kwenye kazi ile unapata siku za furaha kidogo kuliko siku za maudhi lakini cha umuhimu ni wewe kuwa na moyo wa uvumilivu na ustahimilivu,mpaka sasa anaendesha nchi vizuri na changamoto hazikosekani,”amesema na kuongeza

” Nilisema wakati mmoja kwamba Babu yangu alinisumulia kuwa nchi haipoi kama ugali, ugali ukichelewa kuula unapoa wote,Nchi siku zote haiwi hivyo, hapa pakipoa mara kunaibuka hili mara lile lakini katika yote hayo mpaka sasa analiongoza taifa vizuri,””amesema Rais kikwete

Aidha amesema Rais Samia atapata moyo zaidi akiona wao ambao wapo pamoja nae wanaendelea kumuunga mkono kumuonesha kwamba wapo pamoja, wakiwa pamoja na wenzake anapata moyo wa kukabiliana na changamoto kubwa zilizopo ofisini.