April 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CAF yaahirisha nusu fainali Ligi Mabingwa

CAIRO, Misri

SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu Barani Afrika (CAF) wameamua kuahirisha mechi za nusu fainali za Ligi Mabingwa Afrika ‘Total CAF Campions League’ na zile za Kombe la Shirikisho Afrika ‘Total CAF Confederation Cup’ zilizokuwa zichezwe mwezi ujao.

Mechi hizo zimeahirishwa kutokana na janga la virusi vya ugonjwa wa Corona ambalo hadi sasa limeendelea kuzikumba nchi nyingi za Afrika na dunia kwa ujumla.

Kwa mujibu wa ratiba ya mechi za kwanza za Ligi Mabingwa Afrika zilizopangwa kuchezwa Mei Mosi, timu ya Raja Casablanca ilikuwa mwenyeji wa Zamaleck huku Wydad Casablanca akimkaribisha Al Ahly ambapo mechi za marudiano zilipangwa kuchezwa Mei 8.

Kwa upande wa Kombe la Shirikisho, mechi zao zilipangwa kuchezwa Mei 3 ambapo Pyramids ingeanzia nyumbani kumkaribisha Horoya wakati RS Berkane angekuwa mwenyeji wa Hassania Agadir huku mechi za marudio zikipangwa kuchezwa Mei 10.

Mbali na mechi hizo, lakini pia mashindano kuwania kufuzu kucheza Kombe la Dunia kwa wasichana wenye umri chini ya miaka 17 ‘FIFA Women U-17 World Cup Qualifiers’ zilizopangwa kucheza kati ya Mei Mosi hadi 3 na huku zile za marudiano zikipangwa kuchezwa Mei 15 na 17 hadi pale zitakapopangiwa tarehe nyingine.