April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi wa Benki ya TPB Dkt. Endmund Mndolwa.

Benki ya TPB yazidi kuimarika, yapata faida bilioni 15.9

Na Irene Clemence, TimesMajira

BENKI ya TPB plc imepata faida ya kodi ya shilingi Bilioni 15.9 kwa mwaka unaoishia Disemba 31 ,2019.

Hayo yamesemwa Jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki hiyo, Dkt Edmund Mndolwa katika Mkutano Mkuu wa 28 wa wanahisa wa Benki hiyo.

Amesema, benki hiyo imeimarika kwani imeweza kutengeneza faida kubwa hadi kufikia faida kabla ya Kodi ya shilingi Bilioni 23.0

“Mafanikio haya yaliyopatikana kwa mwaka 2019 yanatokana na juhudi kubwa iliyofanywa na Menejimenti na wafanyakazi chini ya ushauri wa Bodi ya wakurugenzi katika utendaji kazi wa kila siku na kujituma kwa wafanyakazi,” amesema Dkt. Mndolwa

Dkt. Mndolwa amesema, ingawa benki hiyo imekuwa na mtaji mdogo ukilinganisha na benki zingine lakini imeweza kufanya vizuri kwa takribani miaka minne mfululizo katika sekta ya benki.

Kutokana na faida nzuri iliyopatikana kwa mwaka 2019 benki hiyo inatarajia kutoa gawio la fedha taslim kwa wanahisa wake kama sehemu ya faida iliyopatikana.

“Utaratibu huu ni kulingana na sera na taratibu ambazo Benki imejiwekea ili kuendelea kuimarisha uendeshaji wake pamoja na kugawa sehemu ya faida kwa wanahisa,” amesema Dkt. Mndolwa

Kupitia gawio hilo wanahisa wataweza kufarijika kupata gawio la fedha taslim ambapo kwa mwaka huu litaongezeka ukilinganisha na mwaka uliotagulia kwa kadri benki inavyoendelea kujiimarisha na kutegeneza faida zaidi.

Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya TPB , Sabasaba Moshingi amesema, faida iliyopatikana mwaka 2019 imetajwa na uongozi wa Benki hiyo kuwa ni kubwa ambayo haijawahi kufikiwa tangu kuanzishwa wa Benki hiyo.

Moshingi amesema, Benki hiyo itaendelea kujipanga na kutanua shughuli zake za kibenki nchini sambamba na kuweka mikakati madhubuti ya kukabiliana na chagamoto za kiuchumi katika sekta ya fedha.

Aidha ametoa wito kwa wateja wote na Watanzania kwa ujumla pamoja na Taasisi mbalimbali kuendelea kuitumia Benki ya TPB katika kuinga mkono kwenye shughuli zake ili iweze kutimiza malengo yake.