April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

COSTECH kuibua bunifu mtaani kukuza ajira hususan kwa vijana

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

MKURUGENZI wa Tume ya Sayansi na Tekonolojia  (COSTECH) Dkt. Amosi Nungu amesema,Tume hiyo imegundua bunifu nyingi zipo mitaani hivyo zinahitaji kuibuliwa ili kukuza ajira kwa vijana hapa nchini.

Ameyasema hayo katika mjadala kuhusu masuala ya ubunifu ulioandaliwa na (COSTECH) ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya wiki ya Ubunifu yanayoendelea katika uwanja Jamhuri jijini Dodoma.

Dkt.Nungu amesema,maadhimisho yanafanyika kwa  mara ya nane hapa nchini ambayo yamelenga kuibua bunifu pamoja na wabunifu wanaozitengeneza ili kuwaendeleza na kuhakikisha bunifu hizo zinaingia sokoni ili kwenda kutatua changamoto katika jamii.

Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda akifungua mjadala kuhusu masuala ya Ubunifu ulioandaliwa na Tume ya Sayansi na Teknolojia COSTECH

“Tumekuwa tukifanya maonyesho haya kwa mara ya nane sasa,.na tumegundua bunifu nyingi bado zipo mitaani na zinahitaji kuibuliwa.”amesema Dkt.Nungu na kuongeza kuwa

” COSTECH tumeamua kufanya midahalo ambayo inaonekana moja kwa moja  ili wabunifu wengi na Watanzania waweze kuona fursa za masuala ya ubunifu ili waweze kuzichangamkia na kutatua changamoto ya ajira nchini.”amesema Mkurugenzi huyo

Akifungua mdahalo huo,Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda amesema Serikali ina jukumuku la kuwajengea wabunifu mazingira mazuri yatakayochochea ubunifu ili kuongeza idadi yao na bunifu hapa nchini.

“Serikali inatambua jitihada zinazofanywa na wabunifu,kwa hiyo tunalo jukumu la kuhakikisha tunawaendeleza lakini pia kuendeleza bunifu zao .”amesema Profesa Mkenda

Amesema kuwa ubunifu sasa umekuwa ukifanywa na watu mbalimbali wakiwemo wasomi na hata watoto huku akitolea  mfano Mtoto mwenye umri wa miaka 10 ambaye yupo kwenye maonyesho hayo aliyegundua  mfumo wa kugundua mtu anayeingia chumbani lakini pia kujua idadi ya walioingia .

“Mbali na hawa wabunifu waliofika kwenye maonyesho haya lakini huko mtaano bado kuna wabunifu wengine  ambao hungundua vitu vingi .”amesisitiza Waziri huyo

Waziri wa Sayansi,Teknolojia na Ubunifu Profesa Adolf Mkenda akifafanua jambo mbele ya waandishi wa habari jijini Dodoma

Amesema kuwa ilani ya CCM inasema wanaofanya vizuri wapelekwe nje wakaendelezwe  kwenye vyuo vya nje ya nchi.

Kwa mujibu wa Waziri huyo Serikali inatenga fedha kwa ajili ya kuwaendeleza wabunifu ili nchi iweze kuwa na vitu inavyotengeneza hapa nchini badala ya kutegemea kila kitu kuagiza kutoka nje ya nchi .

Pia amesema kuwa kwa miaka 10, ijayo Tanzania itakuwa imepita hatua kwenye masuala ya Teknolojia na ubunifu huku akisema,zama za sasa ni za Sayansi na Teknolojia na sekta ya umma inatakiwa kutenda kazi kwa ubunifu ili kuchochea mabadiliko kwenye utendaji kazi.