April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wizara ya Elimu yateta na Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii


Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma


Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknoloja  imefanya kikao na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa lengo la kutoa taarifa ya maendeleo ya kazi ya uboreshaji Mitaala katika ngazi zote za elimu nchini.

Kikao hicho kimefanyika jana Bungeni jijini hapa ambapo uwasilishwaji wa taarifa hizo umefanywa na Wakuu wa Taasisi zinazohusika na mitaala nchini ambao ni Dkt. Aneth Komba kutoka Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), ambaye aliwasilisha kwa upande wa Mitaala ya Elimumsingi, Mtendaji Mkuu Baraza la Elimu ya Ufundi (NACTE) Dkt. Adolf Rutayuga ambaye aliwasilisha uboreshaji wa Mitaala ya elimu ya ufundi na Vyuo vya Kati na Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu (TCU)Tanzania Profesa Charles Kihampa aliewasilisha kuhusu Mitaala ya Elimu ya Juu.

Baada ya mawasilisho hayo Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Stanlaus Nyongo amesema lengo la Kikao hicho ilikuwa ni kupata taarifa ya maendeleo ya zoezi la uboreshaji wa mitaala hiyo ili Kamati yake iweze kurejesha taarifa hiyo kwa wabunge wengine.
Aidha,amesema pamoja na kwamba mchakato bado unaendelea wa kuboresha mitaala ya elimu, kazi hiyo imefanyika na inaonekana ingawa bado haijafika mwisho. 
Mwenyekiti hyo ametumia nafasi hiyo kuitaka Wizara kuwasilisha taarifa hizo kwa Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Novemba 11, 2021 ili nao waweze kutoa maoni.