April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wizara ya Ardhi yazindua kituo cha huduma kwa wateja

NaJoyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

WIZARA ya Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi,imezindua kituo cha huduma kwa wateja kitakachowawezesha wananchi kutoa kero zao ,maoni au ushauri kuhusiana na masuala ya ardhi.

Akizungumza na waandishi wa habari Mtumba jijini Dodoma muda mfupi kabla ya kuzindua kituo hicho,aliyekuwa Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi amesema,lengo kituo hicho ni kurahisisha huduma za masuala yote ya Ardhi lakini pia kusogeza huduma hiyo karibu na wananchi na hivyo kuwapunguzia gharama za kufuata huduma hiyo kwenye ofisi za Ardhi wilaya,mkoa au Makao Makuu.

Amesema,kituo hicho pamoja na mambo mengine kimefunguliwa  kufuatia maendeleo ya Teknolojia ya Mawasiliano na habari yaliyopo kwa sasa lakini pia  kwa kuzingatia hatua stahiki za kujikinga na UVIKO 19.

Lukuvi amesema,wizara hiyo imeona kuwa zipo baadhi ya huduma za ardhi zinazoweza kutolewa kwa njia ya simu na mitandao ya kijamii ambazo hazimlazimu mwananchi kufika katika ofisi za ardhi.

“Wizara imeanzisha kituo cha mawasiliano kwa wateja kitakachotoa huduma ya mawasiliano moja kwa moja na wananchi na kwa kutumia ujumbe wa maneno (Watsapp ) na kutoa majibu au ufafanuzi kwa wananchi hao.”amesema na kuongeza kuwa

“Kituo hiki kina wataalam wabobezi katika masuala yote ya ardhi waliopata mafunzo yakinifu ya kuifanya kazi ya kutoa huduma kwa weledi na kutoa majibu kwa wananchi kuhusiana na masuala yote ya ardhi,katika kupata hiyo mteja  atalazimika kupiga simu na kuongea moja kwa moja na watoa huduma zetu kupitia namba ……

“Nawaasa  wananchi kukitumia  kituo hiki kutoa taarifa zote na kuuliza kila aina ya swali kuhusiana na masuala ya ardhi …,katika mfumo wa Wizara tunao  wataalam kuanzia wilayani mpaka mkoani ,pengine kuanzia huko umepata huduma isiyoridhisha,tupe taarifa huduma gani au nani amekuhudumia vibaya tupe taarifa,

“Pia zipo kero nyingi,umenyang’anywa shamba lako,umenyang’anywa kiwanja hujalipwa fidia tupe taarifa ili utusaidie sisi hapa wizarani tuweze kufuatilia hayo mambo ambayo umeshindwa huko katika wilaya au mkoa,lakini pengine kutokana na teknolojia ya ulipaji kodi wapo wanahangaika katika ulipaji kodi sasa hivi tunalipa kodi kwenye simu pengine unashindwa namna ya kufanya ili uweze kulipa kodi kwa wakati,tuulize tutakujibu.”amesisitiza

Vile vile amerejea kauli yake kuhisna na madalali ambao wamekuwa wakitafuta wateja wa nyumba au mashamba na kasha kulipwa pande zote mbili huku akisema,alishatoa onyo kwa kuwaagiza madalali kuchukua pesa upande mmoja tu wa mmiliki na siyo vinginevyo.

“Kuna matapeli ndani ya mikoa ambao wanatoa huduma lakini kwa namna ambayo haiwaridhishi wananchi,hivi karibuni nimepiga marufuku kwa wananchi kutoa pesa kwa madalali kwa ajili ya kutafutiwa nyumba,tumetoa muongozo kwamba kila mwenye nyumba amlipe dalali ambaye anamtafutia mteja ,sasa wapo baadhi ya madalali wasio waaminifu bado wanaendelea kudai kodi kwa wale wanaowatafutia nyumba ,ni kosa na tunaomba kupitia kituo hiki tupate taarifa zao ili tuendelee kuchukua hatua stahiki dhidi yao.”