May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri wa Uchukuzi wa Japan kufanya ziara na ujumbe wa watu 40 nchini

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Waziri wa Ardhi, Miundombinu, Uchukuzi na Utalii wa Japan, Konosuke Kokuba anatarajia kufanya ziara ya kikazi nchini mnamo mwezi Januari mwaka 2024.

Katika ziara hiyo, Kokuba ataongozana na ujumbe wa watu 40 kutoka kampuni binafsi zinazojihusisha na masuala ya miundombinu na baadhi ya watumishi wa Wizara yake.

Ziara hiyo imelenga kujadili fursa mbalimbali zinazotokana na ushirikiano kati ya Tanzania na Japan katika maendeleo ya miundombinu.

Hayo yamejulikana (07/12/2023) katika kikao cha pamoja cha maandalizi ya ziara hiyo kilichoshirikisha viongozi wa Wizara ya Uchukuzi na Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Bwana Plasduce Mbossa pamoja na Menejimenti yake kilichofanyika jijini Dar es Salaam na kuongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara.

Kwa upande wa Japan, ujumbe wake umeongozwa na Bwana Yoshihiro Kakishita kutoka Sekretarieti ya Wizara ya Ardhi, Miundombinu, Uchukuzi na Utalii ya Japan.

Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Plasduce Mbosaa ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wafanyabiashara na wawekezaji kutoka Japan kuja kuwekeza kwa upande wa miundombinu ya Bandari nchini.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara akimpa zawadi mgeni wakeBwana Yoshihiro Kakishita kutoka Sekretarieti ya Wizara ya Ardhi, Miundombinu, Uchukuzi na Utalii ya Japan wakati wa kikao hicho ambacho kiliongozwa na Katibu Mkuu huyo.Kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Bwana Plasduce Mbossa