April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri Jafo: Miradi iwe na mifumo ya uvunaji maji ya mvua

Na Robert Hokororo, TimesMajira Online,Dodoma

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira),Selemani Jafo ameelekeza miradi ya ujenzi wa nyumba iwe na mifumo ya uvunaji wa maji ya mvua ili kunusuru athari za mafuriko.

Amemuagiza mkandarasi anayetekeza ujenzi wa mradi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Iyumbu jijini Dodoma kujenga mfumo wa uvunaji maji ili yasitiririke na kusababisha athari za kimazingira katika Mji wa Dodoma.

Jafo ametoa maelekezo hayo jana alipofanya ziara ya kikazi katika mradi huo wa ujenzi ya kukagua uzingatiaji wa Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004.

Hata hivyo,ameonesha kutoridhishwa na kukosekana kwa mifumo ya uvunaji maji na kuelekeza uongozi unaosimamia mradi kushirikana na mamlaka zinazohusika na masuala ya usimamizi wa maji kuhakikisha wanajenga mifumo hiyo.

“Hapa sioni mifumo ya uvunaji wa mvua haya mabati yatamwaga maji mengi na kusababisha mafuriko leo hii kule Nkuhungu nyumba zimezama kwa mafuriko, soko la Ndugai na stendi ya Dodoma na maeneo mengine yatajaa maji sasa tukiwe system ya uvunaji maji tutapunguza mafuriko na pili tutafanya management (usimamizi) ya maji,” amesema.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Selemani Jafo (wa tatu kushoto) akiwa katika ziara ya kukagua uzingatiaji wa Sheria ya Mazingira katika ujenzi wa nyuma Iyumba jana jijini Dodoma. Kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri.

Pamoja na hayo pia alizitaka mamlaka zinazohusika na utoaji wa vibali vya ujenzo kuhakisisha vibali hivyo vinawataka waombaji kujenga mifumo ya uvunaji maji katika miradi hiyo ili kuzuia maji yasitiririke ovyo na kusababisha uharibifu wa mazingira katika maeneo ya miji.

Katika hatua nyingine Waziri Jafo katika ziara hiyo iliyolenga kukagua uzingatiaji wa uhifadhi wa mazingira alitoa maelekezo kwa wakandasi kuhakikisha wanapanda miti katika maeneo ya miradi wanayojenga.

Amesisitiza kuwa kuwa agenda ya mazingira iwe kipaumbele cha kwanza katika miradi mikubwa inayotekelezwa nchini na kwamba wakati wa maandalizi ya utekelezaji wa mradi huo, eneo hilo lilifyekwa miti hivyo kuna ulazima wa kupanda miti kwa wingi ili kuliweka katika mazingira mazuri.

”Hizi projects (miradi) kubwa wakati mnazitekeleza lazima agenda ya mazingira iwe kipaumbele cha kwanza kwasababu ukiangalia hili eneo hapa msipopanda miti litakuwa ni eneo la ajabu sana, hapa kwanini msipande miti ya matunda mtu atapata embe na wakati huo anakuta mmetunza mazingira,” alisema.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Dodoma,Jabir Shekimweri amesema pamoja na mradi huo wa nyumba kuwa ni mzuri lakini una changamoto mbalimbali.

Amesema miongoni mwa changamoto hizo ni kutokufuatwa kwa masharti ya mkataba wa ujenzi ambao ni kumtaka mkandarasi pamoja na mshauri kufanya kazi bega kwa bega na wadau kama Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA) ili kupata ushauri usimamizi wa maji.

Shekimweri amesema kuwa ipo haja sasa wakati wa utoaji wa vibali vya ujenzi kuwataka waombaji kupanda mitano ikiwemo ya matunda na ya kivuli ili kuhifadhi mazingira.

Pia ameiomba Serikali kupitia kwa Waziri kuelekeza wakandarsi kusimamiwa kipengele cha kushirikisha wadau muhimu wakiwemo Jiji wakati wa utekelezaji wa miradi ili kuepuka madhara ya kimazingira yanayoweza kutokea.

Naye Mkurugenzi wa Ujenzi wa NHC,Bw.Haikameni Mlekio amesema wameyapokea maelekezo ya Waziri Jafo na kuahidi Uongozi wa Shirika hilo utayafanyia kazi.

Katika ziara hiyo Waziri Jafo aliambatana na Meneja wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC),Meneja kutoka Wakala wa Misitu Tanzania (TFS)-Dodoma,Patricia Manongi na Afisa Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais, Dkt.Deogratius Paul na Afisa kutoka NEMC, Bw. Emmanuel Mwasilu.