March 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri wa Madini, Doto Biteko akiwaonesha jambo viongozi wa serikali na wafanyakazi wa mgodi wa GGML waliopo nyuma yake baada ya kuwasilishwa taarifa ya mgodi huo na Makamu wa Rais wa Mgodi huo, Simon Shayo aliyeshika kipaza sauti kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Robert Gabriel. (Picha na Issa Mtuwa-WM).

Waziri Biteko:GGML mnafanya mambo mengi mazuri, lakini ‘local content’ hainiridhishi

Ataka huduma za kibiashara mgodini wazawa wapewe kipaumbele

Na Issa Mtuwa-WM, Geita

WAZIRI wa Madini, Doto Biteko amesema yapo mambo mengi yanayozungumzwa na kukubaliana kati ya Serikali na Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGML) hususani ulipaji wa kodi na utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya jamii (CSR), lakini bado baadhi hakubaliani nayo hususani suala la utekelezaji wa masuala ya utoaji huduma za kibiashara (Local Content), kwani nafasi hiyo ndio inayowapa wazawa kushiriki shughuli za uchumi kupitia Sekta ya Madini.

Hayo ameyasema mkoani Geita baada ya kuutembelea mgodi huo mkubwa wa Dhahabu wa Geita (GGML) ili kukagua shughuli zinazofanywa mgodini hapo.

Waziri wa Madini, Doto Biteko (katikati) akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Robert Gabriel kulia na Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Prof. Idrisa Kikula kushoto. (Picha na Issa Mtuwa-WM).

Amesema, fursa za watu kushiriki katika utoaji huduma za kibiashara mgodini, ni muhimu kuwapa fursa wazawa ili kuinua uchumi wao na taifa.

Ameongeza kuwa, kazi zinazoweza kufanyika mgodini lazima zifanywe na Watanzania na kwamba kitendo cha hoja ya GGML kutaka kutoa huduma za kufanya tathmini za uingizaji umeme mgodini hapo, hawezi kuidhinisha, vinginevyo Wizara ya Nishati iseme hakuna mtaalam hapa nchini wa kufanya kazi hiyo.

Biteko amezungumzia pia, kuhusu haki ya wananchi hasa kwenye migogoro ya fidia. Aliongeza kuwa, hayupo tayari kuona hata mtu mmoja anadhulumiwa haki yake inayopitia sekta ya madini.

“Manyanyaso ya wanyonge yanayotokana na sekta ya madini, yananiumiza sana, inaniuma kwa sababu, hata aliyenipa mamlaka haya, aliniambie nije kutatua kero za wananchi kwenye sekta ya madini,”amesema Biteko.

Anabainisha kuwa, kijiji cha Magema wananyanyasika kuhusu mahali wanapoishi, huku mgodi ukihitaji eneo hilo, toka walipoomba walipwe fidia mpaka leo na jambo hilo halijatekelezwa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Robert Gabriel amesema, ameteua kamati ya wataalam mbalimbali kufuatilia na kuweka mpango mkakati utakaowahusisha wananchi katika kutoa huduma za kibiashara mgodini hapo kutoka asilimia 31 hadi asimilia 80, huku akiwa tayari kwenda Magema kufanya tathmini ya uhakiki nani mwenye haki na nani asie na haki ili utekelezaji wa fidia ufanyike.

Waziri wa Madini, Doto Biteko akiwaonesha waandishi wa habari baadhi ya mambo yaliyowasilishwa kwake na Makamu wa Rais wa Mgodi wa GGM, Simon Shayo. (Picha na Issa Mtuwa-WM).

Makamu wa Rais wa Mgodi wa GGML, Simon Shayo amesema, mgodi wao upo siku zote kushirikiana na kutekeleza maelekezo ya serikali. Kuhusu utekelezaji wa maagizo ya serikali kuhusu suala la umeme, Local Content na tathimini ya fidia yatazingatiwa.

Shayo ameongeza kuwa, kuhusu ajira na Local Content, mgodi huo unatekeleza vizuri sana huku jumla ya wafanyakazi zaidi ya 4000 wameajiriwa mgodini hapo huku upatikanaji wa huduma za kibiashara za Watanzania imefikia asilimia 31.