April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kamanda wa Polisi mkoa wa Geita, ,Kamishna Msaidizi Mtatiro Kitinkwi akionyesha waandishi wa habari dola za Kimarekani bandia zilizokamatwa na Polisi wakati watuhumiwa wawili wakitaka kuzibadilisha (Picha na Mutta Robert).

Polisi wakamata wawili wakiwa na dola bandia wakijiandaa kufanya miamala Benki ya Azania

Na Mutta Robert,TimesMajira Online, Geita

Jeshi la Polisi Mkoa wa Geita limefanikiwa kukamata watu wawili wakiwa na noti bandia dola za kimarekani 2,100 zenye thamani ya sh.4,861,500 kwa fedha za kitanzania wakiwa kwenye harakati za kufanya miamala katika Benki ya Azania tawi la Katoro.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Kamishna Msaidizi Mtatiro Kitinkwi akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo ofisini kwake amesema kuwa, jeshi hilo lilikamata watuhumiwa wawili waliokuwa wanajihusisha na biashara hiyo ya fedha bandia huku mtuhumiwa mmoja akifanikiwa kutoroka na anaendelea kusakwa na jeshi hilo.

Amesema kuwa, watuhumiwa hao wakiwa kwenye harakati za kubadilisha fedha hizo,Benki ya Azania iliweza kugundua fedha hizo kuwa ni bandia na kutoa taarifa polisi na kufanikiwa kuwatia mbaroni na mmoja kutoroka.

Watuhumiwa wote waliokamatwa wameelezwa kuwa ni raia wa Tanzania na wako mikononi mwa jeshi hilo kuendelea na mahojiano na wanatarajiwa kufikishwa mahakamani baada ya taratibu za kisheria kukamilika.

Kamanda Mtatiro Kitinkwi amesema kuwa, Jeshi la Polisi mkoa wa Geita limefanya operesheni maalum kuanzia tarehe 1 Juni hadi 29 Juni mwaka huu na kufanikiwa kukamata watuhumiwa wa makosa mbalimbali 52 ambao uchunguzi na mahojiano yanaendelea ili waweze kufikishwa mahakamani.